AKINA mama wajasiriamali wametakiwa kuchangamkia fursa zinazojitokeza badala ya kukaa nyumbani na kuwategemea waume zao kwa kila jambo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma …. (endelea).
Ushauri huo umetolewa na Katibu tawala wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Fatuma Mganga alipokuwa akifunga mafunzo ya Jukwaa la uwezeshaji wanawake kiuchuni mkoani Dodoma na kuratibiwa na Taasisi ya Uongozi.
Dk Fatuma amesema ni wakati mwafaka kwa akina mama kuchangamkia fursa za kufanya biashara na kujiingizia kipato.
Amesema kuwa ipo mifuko 61 ambayo akina mama wanaweza kuitumia kukopa kwa lengo la kuhakikisha wanakuza mitaji na kufanya biashara mbalimbali kwa lengo la kujiongezea kipato wao, familia na taifa kwa ujumla.
“Lakini bado kuna asilimia 10 ambayo inatolewa na Halmashauri na hizo zote ni fursa, jamani akina mama tujitokeze kupata fedha na tuweze kufanya mambo makubwa.
“Akina mama wamekuwa waoga katika kufanya shughuli za ikiwa ni pamoja na kuogopa kukopa, wanabaki kujisifia kuwa kwa sasa tuna Rais mwanamke maneno hayo ya kujisifu bila kuwa na hela hilo ni tatizo.
“Nataka niwaambie akina mama wenzangu ni lazima tufanye kazi za kujiongezea kipato na ili uwe na heshima au maziki yawe ya kifahari ni lazima uwe na hela” ameeleza Dk. Fatuma.
Pamoja na mambo mengine Dk. Fatuma ametoa maelekezo kwa Jukwaa hayo na kutoa muda wa siku 30 kuhakikisha wanahuisha majukwaa kila kata na wilaya.
Pia ametoa maagizo ya kuhakikisha inapofika mwezi Februari mwaka kesho Jukwaa la Mkoa liwe limehuishwa huku akitaka majukwaa yanakuwa na katiba, kuwepo kwa mpango mkakati wa kazi.
Katika maagizo hayo pia ametaka viongozi kuhalikisha wanatembelea vikundi vyote vilivyokopeshwa ili kuvibaini na kuhakikisha vinafanya vizuri katika suala zima la uzalishaji.
Leave a comment