MAGARI matatu likiwemo la abiria (daladala) yamegongana katika taa za barabara eneo la Serengeti – Chang’ombe jijini Dar es Salaam na kusababisha vifo vya watu watano palepale na wanane kujeruhiwa. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke jijini Dar es Salaam, Amon Kakwale akizungumza na waandishi wa habari kuhusu ajali hiyo amesema, imetokea saa kumi kasoro asubuhi ya leo Jumatatu tarehe 5 Oktoba 2020.
Amesema, ajali hiyo imetokea katika makutano ya barabara itokayo Tazara kwenda Uhasibu na barabara inayotoka Temeke kwenda Kariakoo.
“Yamekutana katika mataa, yalisababisha ajali ambayo imesababisha vifo vya watu watano wamepoteza maisha pale pale na bado hatujafahamu majina yao na miili yao imehifadhiwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH),” amesema.
Amesema, majeruhi walipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Temeke kwa matibabu zaidi huku madereva wa magari hayo wakikimbia ambapo Kamanda huyo amewataka kujisalimisha kituo chochote cha polisi kwa tararibu zingine.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano cha MNH, Aminiel Aligaesha amesema, hospitali hiyo wamewapokea majeruhi watano kutoka Hospitali ya Rufaa ya Temeke waliopata ajali.
Amewataja majeruhi hao ni; William Paul Akida (42), Alicia Teophil (25),
Valentino Lucas (29) huku wawili majina yao hayajafahamika.
Leave a comment