JINAMIZI la ajali limeendelea kuandama mkoa wa Mbeya baada ya watu watano kufariki dunia na wengine 28 kujeruhiwa baada ya gari aina ya Coaster lililokuwa likisafirisha maiti kutoka Jijini Dodoma kwenda Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya kwa mazishi, kugongana uso kwa uso na basi la Kampuni ya Kyela Express lilikokuwa likitokea Kyela kuelekea Jijini Dar-es-Salaam.
Ajali hiyo imetokea leo Jumanne tarehe 11 Oktoba , 2022, saa 2:00 asubuhi katika kitongoji cha Kanyegere kijiji cha Ibula Kata ya Kiwira Wilaya ya Rungwe Mkoa wa Mbeya. Anaripoti Kenneth Neleti, Mbeya …(endelea).
Akizungumzia ajali hiyo Mkuu wa Wilaya ya Rungwe, Dk Vicent Anney amekiri kutokea na kwamba kati ya watu waliopoteza maisha ni pamoja na dereva wa Coaster.
Dk. Anney amesema kuwa taarifa za awali zinaonesha madereva wote walikuwa na makosa kwani walikuwa mwendo kasi na walitaka kulikwepa lori la mizigo lililokuwa barabarani na kusababisha kugongana uso kwa uso na kusababisha vifo vya watu wawili papo hapo na majeruhi.
Akizungumza kwa njia ya simu Mganga Mkuu Wilaya ya Rungwe Dk Diocles Ngaiza amesema kuwa majeruhi wa ajali walikuwa 28 kati ya hao 14 walipelekwa katika hosptali ya Kanisa Katoliki ya Igogwe na baadaye watatu walipoteza maisha wakati wakiendelea kupatiwa matibabu.
Dk. Ngaiza amesema kuwa mmoja kati ya majeruhi waliosalia alionekana kuwa na hali mbaya zaidi na ndipo ikalazimu kumkimbiza katika Hospitali ya Rufaa Kanda Mbeya.
Ameongeza kuwa katika hosptali ya Wilaya alipokea majeruhi 17 kati hao wanawake 13 wanaume wanne na watu waliopoteza maisha wakiwa wawili na jumla ya vifo vilivyotokana na ajali ni vitano na majeruhi 28.
Leave a comment