WATU wanne wamepoteza maisha huku 26 wakijeruhiwa katika ajali ya basi la abiria la Safari Njema likitokea Dar es Salaam lilipogongana na Lori usiku wa kuamkia leo tarehe 16 Agosti 2019, katika eneo la Nanenane mkoani Morogoro. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Akizungumzia kuhusu ajali hiyo Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Wilbroad Mutafungwa amesema, miongoni mwa watu wane waliopoteza maisha ni dereva wa Lori ambaye jina lake halijafahamika mpaka sasa.
Kamanda Mutafungwa amesema, majeruhi walikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro kwa ajili ya matibabu, na kwamba majeruhi 23 wameruhusiwa kutoka kutokana na hali zao kuimarika ambapo watatu wanaendelea kupata matibabu.
“Watu wane wakapoteza maisha, abiria wengine walikimbizwa hospitalini kwa ajili ya kupatiwa matibabu, wengine wameruhusiwa kutoka, watatu bado wako hospitali wakipatiwa matibabu,” amesema Kamanda Mutafungwa na kuongeza;
“Abiria wengine walipelekwa hospitali, idadi kubwa wametibiwa wameondoka, wamebaki abiria watatu hali zao zinaendelea vizuri wameendelea kupatiwa matibabu kwenye hospitali ya Rufaa Morogoro.”
Kamanda Mutafungwa amesema, chanzo cha ajali hiyo ni dereva wa basi la abiria lenye namba za usajili T 212 DNU lililokuwa linatokea jijini Dar es Salaam kuelekea mkoani Dodoma kuendesha kwa uzembe kwa kutaka kulipita gari lingine pasipo kuchukua tahadhari.
Amesema, baada ya dereva huyo kufanya uzembe, aligongana ubavu na lori lenye namba za usajili T 802 DWU ambalo ni mali ya Kampuni ya Tumbaku Alliance.
“Ni kweli usiku wa kuamkia leo majira ya saa saba na nusu usiku, kwenye barabara kutoka Dar es Salaam kuingia Morogoro, ilipofika kwenye eneo la tukio dereva ali ‘overtake’ bila kuchukua tahadhari ya kutosha, akagongana kiubavu na lori aina ya Tata mali ya kampuni ya Tumbaku,” amesema Kamanda Mutafungwa.
Kamanda Mutafungwa amesema, Jeshi la Polisi linamsaka dereva wa basi hilo ambaye alitoroka baada ya kutokea ajali hiyo, huku akisisitiza kwamba kama hawatafanikiwa kumpata, watamtafuta mmiliki wa basi hilo ili atoe ushirikiano wa namna ya kumpata mtuhumiwa huyo.
Aidha, Kamanda Mutafungwa ametoa wito kwa madereva kuchukua tahadhari sambamba na kufuata sheria za usalama barabarani ili kuepusha ajali zinazogharimu maisha ya watu.
“Madereva wanaoendesha usiku waendelee kuchukua tahadhari ili kuepuka ajali, kuruhusiwa kutembea usiku isiwe sababu ya kwenda bila kuzingatia sheria za usalama barabarani,”amesema Kamanda Mutafungwa.
Hivi karibuni ilitokea ajali ya lori la mafuta mkoani Morogoro iliyopoteza maisha ya watu 89 na kuacha majeruhi zaidi ya 40.
Leave a comment