WAIMBA taarabu maarufu nchini Tanzania, Aisha Ramadhani maarufu Aisha Mashauzi, Hadija Kopa na Mzee Yusuph watalitikisa Jiji la Dodoma Jumamosi hii tarehe 27 Novemba 2021, katika tamasha la taarabu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Tamasha hilo, litafanyikia katika viwanja vya mapumziko vya Chinangali Park jijini humo.
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu tamasha hilo, Aisha Mashauzi kwa niaba ya waimbaji wenzake, aliawamba wana Dodoma hususani wapenzi wa taarabu kujitokeza kwa wingi kuhudhuria tamasha hilo kwani kutakuwa na mambo mazuri lengo kuu likiwa ni kuamsha mziki huo ambao siku za hivi karibuni umefifia.
Alisema chanamoto kubwa waimbaji wa mziki wa taarabu wamekuwa waoga, kutokujiamini na kujikuta wakishindwa kuutangaza vyema mziki huo.
Alisema yeye ameamua kuvunja ukimya na kuzunguka nchi nzima akifanya tamasha na anaamini uamuzi huo utautambulisha na kuuibua upya mziki huo.
Mashauzi alisema tamasha lijulikanalo kwa jina la ‘International Taarabu Concert’ atazunguka nchi nzima akitoa burudani pamoja na kusaka vipaji.
“Ndugu Watanzania, kila mtu anajua kuwa mziki wa taarabu ulikuwa umefifia lakini kwa sasa nimeamua mimi Aisha Mashauzi au Simba dume kurejesha heshima ya mziki huo.”
“Jumamosi nitakuwa Chinangali Park kuanzia saa mbili usiku hadi saa sita usiku, kutakuwepo nguli wa mziki wa taarabu ambao ni Hadija Kopa na Mzee Yusuphu ambapo viongozi mbalimbali wa Mkoa na wabunge watakuwepo,” alisema
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Chinangali Park na Capetown bar, Frank Ngonyani amesema umefika wakati sasa wa viongozi wa kiserikali na taasisi mbalimbali kuunga mkono mziki wa taarabu.
Mbali na hilo, Ngonyani alisema kitendo cha Mashauzi kuwa na fikra za kuibua vipaji ni sehemu ya kuwafanya vijana kuachana na maisha ya kukaa vijiweni na badala yake watambue kuwa mziki au sanaa ni sehemu ya ajira.
“Nataka niwaambie Watanzania pamoja na viongozi mbalimbali watambue kuwa sanaa yoyote nchini ni sehemu ya ajira hivyo tusisahau kuibua vipaji vya vijana wetu” alisema Ngonyani.
Leave a comment