RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amelitaka Jeshi la Polisi kuacha kutumia nguvu kubwa katika utekelezaji wa majukumu yake ili kuondoka na aibu ya watuhumiwa kufia mikononi mwao. Anaripoti Gabriel Mushi, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ametoa agizo hilo leo Jumatano tarehe 25 Agosti, 2021 wakati akifungua kikao kazi cha maofisa wakuu waandamizi wa jeshi la polisi na makamanda wa polisi wa mikoa/vikosi – Oysterbay Dar es salaam.
“Kumekuwapo na matumizi makubwa ya nguvu. Hili nalo naomba mlitizame…kesi za watu kufariki kwenye vituo vya polisi haipendezi machoni kwa watu, tendeni yaliyo haki,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema kuna watuhumiwa wengine ni ngangari hata kama askari akimchapa virungu vya kutosha lakini kuna wengine virungu viwili tu amepoteza maisha.
Amesema baadhi ya askari wanashutumiwa kutofanya haki kwa jamii na inapotokea wakakiuka maadili ya kazi wanasimama haraka kujitetea kama jeshi bila kuangalia haki za jamii.
“Kwa mfano miezi miwili mitatu nyuma kulikuwa na unyang’anyi wa nyama kwenye mabucha hapa Dar, Polisi mlipolalamika mkasema tumefanya vile kwa sheria, lakini ukiangalia kilichotendeka hakuna sheria hapa, muangalie na hili, mpo hapa kuhudumia watu,” amesema.
Leave a comment