WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba ameiagiza Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kufuata sheria na taratibu za nchi katika ukusanyaji mapato, pasi na kuwaathiri walipakodi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Dk. Mwigulu ametoa agizo hilo leo Jumamosi tarehe 3 Aprili 2021 jijini Dodoma, akizungumza na watendaji wa taasisi na idara zilizoko katika Wizara ya Fedha na Mipango.
“Sheria zipo, taratibu zipo na zoezi hili linafanywa na wataalamu ambao wabobezi. Turekebishe pale ambapo tumeenda kinyume na sheria na weledi wetu, turudi kweye mstari ili tulinde uchumi wetu vilevile tusiuwe walipa kodi,” ameagiza Dk. Mwigulu.
Agizo hilo ni utekelezwaji wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan alilolitoa hivi karibuni kwa wizara hiyo, akiitaka isiwabebeshe mzigo mkubwa walipa kodi, ili kuzuia baishara kufungwa kutokana na wafanyabaishara kushindwa kulipa kodi hizo.
“Ili tuweze kuendelea kupata mapato makubwa katika nchi yetu ni lazima tukuze uchumi, lazima uchumi uwepo ndiyo tunaweza kupata mapato, rais hili aliliangalia na kulipa uzito mkubwa kwamba lazima tulinde uchumi wetu, maana yake tukuze uchumi wetu tutapata wigo mpana kukusanya kodi,” amesema Dk. Mwigulu.
Waziri huyo wa fedha amesema “Sisi wizara pamoja na taasisi lazima tulifanyie kazi na tutekeleze ipasavyo, kwa hiyo kila mtu kwa idara yake ajipange nalo na liwe kiapumbele, tukuze uchumi tuzalishe walipa kodi.”
Leave a comment