LINNA Romani Maro (47), amehukumiwa kifungo cha miaka 30 gerezani na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, baada ya kukutwa na hatia ya kusafirisha madawa ya kulevya. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Katika Kesi ya jinai Na. 295/2018, Maro alitiwa hatiani baada ya mahakama kujiridhisha na ushahidi uliowasilishwa mbele yake na upande wa mashitaka.
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Agustina Mbando, ameeleza katika uamuzi wake aliyoutoa jana Jumanne, tarehe 2 Februari 2021 kuwa Linna ametiwa hatiani katika kosa la kusafirisha dawa hizo kinyume na kifungu cha 15 cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na madawa ya Kulevya Na. 5 ya mwaka 2015 sheria Na. 15 ya mwaka 2017.
Baro alifikishwa mahakamani baada ya kukamatwa na dawa hizo aina ya Heroin, zenye uzito wa gramu 43.95, mwaka 2018.
Kesi dhidi ya mtuhumiwa huyo, ilifunguliwa mahakamani hapo na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Jumatano na Afisa Mawasiliano wa DCEA, Daniel Kasokola, hukumu hiyo imetolewa jana tarehe 2 Februari 2021 na Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Agustina Mbando.
Mtuhumiwa huyo alikamatwa na DCEA tarehe 26 Januari 2018, maeneo ya Tabata Bima, wilayani Ilala, mkoani Dar es Salaam.
Leave a comment