MAMIA ya wafuasi wa Chama cha upinzani nchini Afrika Kusini – Democratic Alliance wameandamana jana tarehe 25 Januari 2023 kupinga kukatika kwa umeme kunakoendelea hali ambayo inazorotesha uchumi wa nchi hiyo iliyoendelea zaidi barani Afrika. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Afrika Kusini imeghubikwa na tatizo la nishati kwa zaidi ya muongo mmoja, lakini tatizo hilo limeongekeza zaidi mwaka huu, huku nchi hiyo ikikabiliwa na ukosefu wa umeme kila siku – wakati mwingine kwa muda wa saa 10 kwa siku.
Eskom – shirika la umeme la serikali lenye madeni, linakabiliwa na mitambo ya makaa ya mawe iliyochakaa ambayo inadaiwa kuharibika mara kwa mara.
Rushwa na hujuma pia zimelidhoofisha shirika hilo kwa kiasi kikubwa.
Kutokana na hali hiyo, Mkurugenzi Mtendaji, Andre de Ruyter wa shirika hilo anatarajiwa kuacha kazi mwishoni mwa Machi.
Mamia ya waandamanaji walikusanyika nje ya makao makuu ya chama tawala cha African National Congress, wakiilaumu serikali kwa kushindwa kutatua tatizo la umeme.
Mapema wiki hii, Rais Cyril Ramaphosa alisema serikali inaangalia suala la kuingiza umeme kutoka nje, lakini ameonya tatizo hilo haliwezi kutatuliwa kwa siku moja.
Leave a comment