TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imemkamata Afisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Mary Moyo kwa tuhuma za kuomba na kupokea rushwa ya Sh.8 milioni kutoka kwa mfanyabiashara ili aweze kumrekebishia hesabu zake na kumtengenezea ‘control number’ ya deni analodaiwa la Sh.97.1 milioni. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Taarifa iliyotolewa leo Jumatano tarehe 30 Septemba 2020 na Naibu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Mwanza, Daudi Ndyamukama imesema, Mary alitaka kumrekebishia deni hilo ili kufikia Sh.35 milioni.
“Hata hivyo, afisa wa TRA alimshawishi mfanyabiashara huyo alipe kiasi cha Sh.35 milioni kwa makubaliano kwamba kati ya kiasi hicho cha fedha afisa alipwe za kwake Sh.8 milioni ili amtengenezee deni la Shn27 milioni ambayo angelipa kwa control number,” amesema Ndyamukama
Amesema, tarehe 26 Septemba 2020 siku ya Jumamosi Mary Moyo alimpigia simu mfanyabiashara huyo na kumuelekeza afike eneo la St. Dominic Nyakahoja Mtaa wa Balewa Kata ya Isamilo jijini Mwanza ili ampatie kitita hicho cha fedha Sh.8 milioni alizomuomba.
“Rushwa hupofusha waonao, baada ya mfanyabiashara kufika eneo la tukio na kumkabidhi Mary aliyoiomba- Mary aliipokea na kuiweka kwenye begi lake la kompyuta.”
“Mary baada ya kupokea fedha hizo za rushwa ghafla maafisa wa Takukuru walifika katika eneo hilo na kumuweka chini ya ulinzi. Mary alipogundua amekamatwa na maafisa wa Takukuru aliangua kilio huku akiomba kusamehewa,” amesema
Ndyamukama amesema, uchunguzi wa tuhuma huo umekamilika na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani leo Jumatano kujibu mashtaka yanayomkabili.
Leave a comment