CHAMA cha Alliance For Democratic Change (ADC), kimepongeza hatua ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kumteua Naibu Katibu Mkuu wao, Queen Sendiga, kuwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Pongezi hizo zimetolewa leo Jumatatu, tarehe 17 Mei 2021 na Katibu Mkuu wa ADC, Doyo Hassan Doyo, wakati akizungumza na MwanaHALISI Online, kuhusu uteuzi huo.
Jumamosi iliyopita tarehe 15 Mei 2021, Rais Samia alimteua Sendiga kuwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, ikiwa ni utekelezaji wa ahadi yake ya kushirikisha wapinzani katika serikali yake, ili kujenga umoja wa kitaifa.
Akizungumzia uteuzi huo, Doyo amemuomba Rais Samia aendelee kuteua viongozi kutoka vyama vya upinzani, hasa ndani ya ADC.
“Tunampongeza Rais Samia kwa kuona inafaa kufanya kazi na vyama vingine na tunamuomba afanye hivyo, aweze kutafuta tafuta tena.
“Kama atapata ADC itakuwa bora zaidi, lakini kama atapata kwenye vyama vingine, tunaomba watoe ushirikianeo ili kutimiza malengo ya rais ya kufanya kazi na viongozi wengine wa vyama vya siasa,” amesema Doyo.
Alipoulizwa kama chama chake hakihofii kumpoteza naibu katibu mkuu wake huyo, Doyo amesema uteuzi huo hautaathiri ADC, kwani wanamuamini Sendiga, kwamba hawezi kujiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM), baada ya kupata uteuzi huo.
“Kuhusu suala la mtu kuwa mkuu wa mkoa anakwenda CCM, hilo suala halina uhakika sababu kwenda CCM ni matakwa ya mtu, Sendiga tunamuamini ni mtu makini, hakuteuliwa kwa sababu ya kwenda CCM na hata rais alipomteua hakumteua ili aongeze nguvu CCM,” amesema Doyo.

Katibu Mkuu wa ADC amesema ” Rais alimteua sababu alitamka nyuma kwamba mtu mwenye weledi na uwezo atampa nafasi katika Serikali yake, tunaamini Rais Samia hakumteua Sendiga awe MwanaCCM.”
Anna Mghwira, aliyekuwa Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, alihamia CCM mwaka 2017, miezi kadhaa baada ya kuteuliwa na aliyekuwa Rais wa awamu ya tano, Hayati John Magufuli, kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro.
Doyo amesema, uteuzi wa Sendiga kuwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa hautaathiri utendaji wake ndani ya chama, kwa maelezo kwamba, ana uwezo wa kuvaa kofia zote mbili kwa wakati mmoja.
“Sisi hatuna tatizo hilo, mwanzoni tulikuwa waziri (Hamad Rashid) kwenye Baraza la Mapiunduzi Zanzibar na alikuwa mwenyekiti wa ADC, sisi ni watu tunaofanya kazi na chama chochote pamoja na Serikali bila kuathiri mifumo yetu ya uongozi,” amesema Doyo.
Hamad Rashid Mohammed, akiwa Mwenyekiti wa ADC, 2016 aliteuliwa na aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, kuwa Waziri wa Afya, nafasi aliyohudumu hadi Baraza la Mapinduzi la visiwa hivyo lilipovunjwa mwaka jana.
Leave a comment