CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimeutaka Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), kutafakari upya kuhusu bei ya ukarabati wa Kivuko cha MV Magogoni, kikidai kwamba ni kubwa, ikilinganishwa na gharama halisi za matengenezo hayo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa na Waziri Kivuli wa Mawasiliano, Teknolojia ya Habari na Uchukuzi wa ACT-Wazalendo, Mwalimu Philbert Macheyeki.
Msemaji huyo wa sekta ya uchukuzi ACT-Wazalendo, amedai uchunguzi uliofanywa na chama hicho kuangalia ukarabati wa kivuko unafanywa katika vitu gani, umebaini gharama ya ukarabati wake wa Sh. 7.5 bilioni ni kubwa, kwa kuwa idadi ya mashine na giaboksi yenye ukubwa unaohitajika gharama zake haizidi Sh. 2 bilioni.
“Tunaitaka Wizara ya Uchukuzi kupitia TEMESA watafakari upya kuhusu bei ya ukarabati wa kivuko kwani kwa vyovyote vile kivuko kilichotengenezwa kwa Sh. 8 bilioni, kukarabatiwa kwa Sh. 7.5 bilioni inatia ukakasi kwa umma. Mfano kivuko kipya cha MV Mwanza kilichotengenezwa kipya na kampuni ya kitanzania 2018, kimegharimu Sh. 8.9 bilioni tu na kina tofauti ndogo na MV Magogoni,” amedai Mwalimu Macheyeki.
Katika hatua nyingine, Mwalimu Macheyeki ameitaka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU), kuchunguza utaratibu wa utoaji zabuni kwa madai kuwa umegubikwa na rushwa.
“Tunaitaka TAKUKURU kuchunguza upya mchakato wa zabuni kwani tayari ulishakuwa na shaka ya upendeleo na kutofuata sheria,” amedai Mwalimu Macheyeki.
Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, hivi karibuni ilitoa ufafanuzi kuhusu masuala hayo, ambapo ilisema zabuni ya matengenezo hayo ilipatikana kwa kufuata misingi ya sheria.
Kwa upande wa gharama, ilisema ukubwa wake unatokana na kivuko hicho kuwa kutumika kwa miaka 14 bila kufanyiwa ukarabati mkubwa.
Leave a comment