CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimewataka waandishi wa habari na wadau wengine wa tasnia hiyo, kupaza sauti zao ili Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Huduma za Habari ya 2016, uwasilishwe bungeni ili kufanyiwa marekebisho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 9 Februari 2023 na Msemaji wa Sekta ya Habari ACT-Wazalendo, Mwalimu Philbert Macheyeki, akizungumza na MwanaHALISI Online kwa simu, ikiwa ni siku kadhaa tangu Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, kusema muswada huo umeshindikana kuwasilishwa bungeni kutokana na ratiba za mhimili huo kubana.
Mwalimu Macheyeki amewataka waandishi wa habari wasikubali muswada huo kuwasilishwa bungeni kwa njia ya dharura, kwa kuwa utakosa fursa ya kujadiliwa kwa ajili ya kubaini madhaifu yake.
“Wanahabari wajitoe kitanzi walichojiweka kwa kuwa wakali kuhusu Sheria ya Huduma za Habari. Ni dhahiri walikuwa wanadanganywa kwani taratibu za kibunge zilikuwa zinaonyesha dhahiri kuwa muswada usingesomwa mkutano huu wa bunge,” amesema Mwalimu Macheyeki.
Msemaji huyo wa sekta ya habari ACT-Wazalendo amesema “Wanahabari waelekeze nguvu muswada uchapishwe kwenye gazeti la Serikali na kusomwa mara ya kwanza Mkutano wa Aprili ili hatimaye usomwe mara ya pili kwa mjadala Mkutano wa Septemba. Wanahabari wasikubali muswada kufanywa wa dharura kwani kwa njia hiyo umma hautapata muda wa kujadili kwa kina na mapungufu kuboreshwa.”
Katika hatua nyingine, Mwalimu Macheyeki amewataka wanahabari kuhoji sababu za muswada huo kukwama kuwasilishwa bungeni mara kwa mara, ambapo kwa mara ya kwanza Serikali ilipanga kuuwasilishwa katika vikao vya Bunge la Novemba 2022.
“Sisi ACT Wazalendo tutakuwa na wanahabari mpaka dakika ya mwisho kutaka maboresho ya Sheria ya Huduma za Habari,” amesema Mwalimu Macheyeki.
Leave a comment