CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimewaomba Watanzania wakiunge mkono ili kiweze kutimiza malengo yake ya kuwakomboa kiuchumi, kijamii na kisiasa. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa Leo Jumamosi, tarehe 18 February 2023 na Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Juma Duni Haji, katika uzinduzi wa ahadi ya chama hicho kwa Watanzania.
“CCM wamejaribu kila sera lakini bado hatujaona nafasi ya kujiona Tanzania tutakuwaje miaka 60 ijayo. Wananchi tuungeni mkono tufike tunakotaka kwenda badala ya kila siku tunalia,” amesema Babu Duni.
Mwanasiasa huyo amesema, ACT-Wazalendo kina ndoto ya kumaliza changamoto zinazowakabili wananchi hususan upungufu wa maji, chakula, huduma za afya, kilimo na uzalishaji maji.
Babu Duni amesema kuwa, Tanzania ina miaka 60 tangu kupata uhuru lakini haina maendeleo ya kutosha kutokana na kukosa dira.
“Wenzetu duniani wakishaweka taratibu kwamba sera ya mambo ya nje iwe hivi kila Rais atatekeleza sera kwa mujibu wa taratibu ilizojiwekea,” amesema Babu Duni.
Naye Makamu Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Bara, Dorothy Semu, amesema chama chao kimejipambanua kuwa chama cha kutoa suluhisho kuliko kupinga kila kitu.
“Tumefahamu kwa kipindi kirefu nchi yetu imekuwa ikizoea siasa zinazojinasibu kuwa unapinga nini, kuliko unapendekeza nini. Sisi tumekuwa tukifanya siasa za utofauti fukipendekeza suluhisho mbadala kwa masuala yote yanayohusu watanzania,” amesema Semu.
AJALI MBAYA YATOKEA MLIMA WA ACT MZALENDO JIJINI MBEYA