CHAMA cha ACT Wazalendo kimepokea taarifa iliyotolewa na Chama Cha Mapinduzi CCM baada ya Kumalizika Kikao Cha Halmashauri Kuu kilichofanyika jana Dodoma, na Kupitisha Uamuzi wa kuishauri Serikali kufufua na kukamilisha mchakakato wa upatikanaji wa katiba mpya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Katibu wa Habari, Uenezi, Mahusiano na Umma wa ACT-Wazalendo Taifa, Salim Bimani, leo Ijumaa tarehe 23 Juni, amesema chama chake kinapongeza msimamo huo uliopitishwa jana Alhamisi na Halmashauri Kuu ya CCM, kwani umezaa matunda ya mazungumzo ya vyama vya siasa nchini na Serikali.
“Tunapongeza hatua hii kubwa sana. Mwenyekiti wa Taifa wa Chama chetu, Juma Duni Haji, amefarijika kuwa mazungumzo yake na viongozi wakuu wa serikali ya jamhuri ya muungano na ya zanzibar yamezingatiwa katika uamuzi huu. Faraja yetu inatokana na ukweli kuwa mazungumzo tuliyoyasukuma na kuyaenzi yameanza kuonyesha matunda,” amesema Bimani.
Hata hivyo, Bimani amesema ACT Wazalendo kinasisitiza kuwa mchakato wa upatikanaji wa katiba mpya uzingatie maoni ya watanzania waliyoyatowa na kuratibiwa na Tume ya Jaji Joseph Sinde Warioba (Tume ya Warioba).
“ Tunatambua kuwa ni lazima kuwepo na mchakato wa kupata mwafaka wa namna ya kufanikisha mchakato wa Katiba mpya, sisi ACT Wazalendo tayari tumeshawasilisha mapendekezo yetu kwa Kikosi Kazi Cha Rais wa Jamhuri ya Tanzania,” amesema Bimani na kuongeza:
“Tunaamini kuwa Kikosi Kazi kitaratibu maoni na mapendekezo ya Vyama vyote na wadau wengine na kuyafikisha Serikalini ili mchakato wa Katiba mpya uanze ifikapo Mwezi Oktoba kama tulivyopendekeza. Tunatarajia juhudi za kukamilisha mchakato wa kupata katiba mpya na tume huru ya uchaguzi zitakwenda sambamba na kuharakisha mchakato wa maridhiano ya Zanzibar.”
Kwa upande wake Chadema kupitia Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Salum Mwalimu, kimesema kitajadili suala hilo kisha kitatoa kauli yake kwa umma.
“Kuhusu hili la maazimio ya Halmashauri Kuu ya CCM, naomba mtupe muda sababu na sisi kama chama tunapaswa kukaa. Wenzetu walikaa na wao wakasema, na sisi tunaomba tukae ndiyo tuseme isije ikawa sasa kudanda danda,” amesema Mwalimu na kuongeza:
“Wanachama wetu kote waliko waendelee kukiamini chama chao na waendelee kuwa watulivu katika kujadili na kuchambua mambo hayo.”
Leave a comment