CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimeishauri Serikali ya Tanzania, iwasilishe bungeni mpango maalumu wa kunusuru sekta zilizoathirika kiuchumi, kutokana na janga la Ugonjwa wa Korona (UVIKO-19). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumapili, tarehe 8 Agosti 2021 na Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, akihutubia katika kikao cha dharura cha Kamati Kuu ya chama hicho, kilichofanyika visiwani Zanzibar.
“Ninaisihi Serikali kuwasilisha Bungeni mpango maalumu wa kunusuru sekta ambazo zimeumizwa na ugonjwa wa Korona, hususani sekta ya utalii,” amesema Zitto.
Pia, Zitto ameiomba Serikali iweke mkakati maalumu wa uhamasishaji wananchi dhidi ya maambukizi ya Korona.
“Niweke bayana kuwa, ni lazima kuwepo na mkakati maalum wa uhamasishaji dhidi ya Korona ambao utaongozwa na watu wanaoaminika kwenye jamii na sio watu wale wale ambao walituambia kuwa Tanzania imeishinda Korona, ama watu wale wale ambao walituaminisha kunywa malimau na tangawizi ni kutibu Korona,” amesema Zitto.
Zitto ameongeza “hatuwezi kuwa na utekelezaji bora wa sera mpya za kupambana na Korona, iwapo tutaendelea kuwa na sura zile zile zilizotuaminisha kutumia njia zisizoshauriwa kisayansi.”
Mbali na ushauri huo, Zitto ameishauri Serikali iwekeze nguvu katika kuelimisha wananchi juu ya umuhimu wa chanjo ya UVIKO-19.
“Hata hivyo, bado kuna kazi kubwa zaidi ya kufanya kwenye uhamasishaji wa watu kujitokeza kupata chanjo. Nitoe rai kwa kila mmoja wenu, nikianza na wanachama wa ACT Wazalendo kufuata taratibu na kupata chanjo mapema iwezekanavyo,” amesema Zitto.
Zitto amewahimiza Watanzania kupata chanjo hiyo, akisema kwamba ni salama.
“Napenda kuwahakikishia kuwa, nimejiridhisha chanjo zilizoruhusiwa kuingia nchini ni salama na mimi pia nimekwisha chanjwa na niko salama salimini. Nipende kuwaasa kuwa, kuchanjwa ni swala la hiari lakini tunapoangalia usalama wa wapendwa wetu, jamii yetu na watanzania wenzetu basi hatuna budi kuhakikisha tunafanya maamuzi sahihi,” amesema Zitto.
Tunaongozwa na wanafiki ambao jana walituambia hakuna Korona na leo wanatuambia tuchanje. Huu ndio uongozi wa Tanzania