CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimetoa wito kwa watetezi wa haki za binadamu Tanzania kuungana na vyama vya siasa vya upinzani katika harakati za kudai katiba mpya na tume huru ya uchaguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo ulitolewa jana Ijumaa, tarehe 13 Mei 2022 na Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, akizungumza katika sherehe za maadhimisho ya miaka 10 ya Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), ambapo mgeni rasmi alikuwa Rais Samia Suluhu Hassan.
“ACT Wazalendo tunataka Mchakato wa Katiba Mpya uanze sasa, sambamba na mchakato wa Tume Huru ya Uchaguzi. Watetezi wa haki za binadamu tunapaswa kuungana kwenye hili,” alisema Ado.
Aidha, Ado alipongeza jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan, za kufungua uwanja wa siasa na kiraia, huku akishauri suala hilo lijengwe kisheria ili lisiwe hisani.
“Ni kweli uwanja wa kisiasa na kiraia umeanza kufunguka. Leo hii, THRDC wasingeweza kufanya shughuli kama hii miaka michache iliyopita kwa sababu Akaunti zao za Benki zilifungiwa. Kwa hili, tunampongeza Rais Samia,” alisema Ado.
Ado alisema “hata hivyo, ACT Wazalendo hatutaki suala hili liendelee kuwa hisani ya Rais. Tunataka Katiba Mpya ili iweke misingi madhubuti ya kisheria kulinda haki za kisiasa, kiuchumi na kiraia.”
Awali, Ado aliwapongeza THRDC kwa kutimiza miaka 10 tangu kuanzishwa kwake na kazi kubwa wanayoifanya.
“THRDC mnafanya kazi kubwa ya kuwatetea watetezi wa haki za binadamu. Sisi wanasiasa ni sehemu ya wanufaika kwa kupaza sauti kwenu au msaada wa kisheria. Kwenye Ripoti yenu ya miaka 10, kuna matukio kama ya kutekwa kwa Raphael Ongangi, aliyekuwa msaidizi wa Zitto Kabwe, Kiongozi wa Chama),” alisema Ado na kuongeza:
“Kutekwa kwa Abdul Nondo, Mwenyekiti wa Vijana ACT Wazalendo, kukamatwa kwa Vital Maembe, Naibu Msemaji wa Sekta ya Utamaduni, Sanaa, Ubunifu na Michezo. Kwenye matukio yote haya mmefanya kazi kubwa ya kupaza sauti na kutoa msaada wa kisheria. Endeleeni na mapambano kwa kasi zaidi.”
Leave a comment