CHAMA cha Wananchi (CUF), kipo kwenye wakati mgumu baada ya ACT-Waalendo kuendelea kubomoa ngome zake. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Licha ya kauli tata kutoka Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini kwamba, kinaweza kufutwa, chama hicho kimeendelea kupokea waliokuwa wanachama wa CUF kwenye maeneo mbalimbali ya nchi.
Katika jiji la Tanga, Kata ya Duga mamia ya waliokuwa wanachama wa CUF wamechukua kadi za ACT-Wazalendo kwa madai ya kuchoshwa na mwenendo wa Prof. Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa CUF-Taifa na viongozi wengine wa chama hicho.
“Simuelewi Prof. Lipumba na viongozi wenzake, lakini nimechoshwa na mwenendo wa CUF. Naamini katika demokrasia ndio maana najiunga na ACT-Wazalendo,” amesema Godfrey Simon baada ya kuchukua kati ya CUF.
Kutokana na kazi inayofanywa na waliokuwa viongozi wa CUF baada ya kujiunga na ACT-Wazalendo, Ismail Jussa, aliyekuwa kiongozi mwandamizi wa CUF ameandika kwenye ukursa wake wa twetter akiwapongeza viongozi hao kwa kazi ya usajili wa wanachama wapya kutoka CUF.
“Mpambanaji Rashid Jumbe Hamza akiwaongoza waliokuwa wanachama wa CUF wa Kata ya Duga, Mkoa wa Tanga kushusha tanga na kupandisha tanga ili safari iendelee. ACT-Wazalendo ndiyo habari ya mjini,” ameandika Jussa.
Ado Shaibu, Katibu Mwenezi na Mawasiliano ya Umma wa chama hicho ameuambia mtandao wa MwanaHALISI ONLINE kuwa, shughuli za chama hicho hazijakwamishwa na chochote na kwamba, uimara wa hali ya juu wa ACT-Wazalendo sasa unadhihiri.
“Tanga na maeneo mengine ya nchi kazi inaendelea kama ilivyopangwa, wanachama wanaendelea kujiunga. Wao wenyewe wamefurahia ACT-Wazalendo, wamefurahia Maalim Seif Sharif Hamad kuhamia chama hiki,” amesema.
Leave a comment