CHAMA cha ACT Wazalendo kimeitaka Serikali iunde tume huru itakayojumuisha wafanyabiashara wadogo ‘wamachinga’ kuchunguza vyanzo vya masoko kuungua moto.
Pia kimesema tume hiyo itasaidia kuondoa minong’ono kuhusu madai ya masoko hayo kuchomwa moto na wafanyabiashara hao kwa lengo la kupinga kuhamishwa na serikali. Anaripoti Rhoda Kanuti, Dar es salaam… (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 11 Aprili 2022 na Msemaji Sekta ya Waziri Mkuu Kivuli cha ACT Wazalendo, Dorothy Semu wakati akitoa tathmini ya chama hicho kwa waandishi wa habari kuhusu hotuba ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa aliyoitoa bungeni hivi karibuni.
Amesema licha ya Ofisi ya Waziri Mkuu kitengo cha maafa kuunda kamati za uchunguzi pindi yanapotokea matukio ya ajali za moto katika masoko mbalimbali nchini, hadi sasa hakuna matokeo ya uchunguzi wa kamati hizo uliowekwa wazi kuhusu ajali hizo.
Semu amesema chama hicho kinashangaa, kwamba katika hotuba ya Waziri Mkuu aliyoisoma bungeni jijji Dodoma haijaonyesha matumaini yeyote ya kuipa nguvu idara ya maafa ili kuzuia masoko kuungua na majanga mengine.
Aidha, amesema ili kukabiliana na maafa hayo lazima kufanyike uchunguzi huru kuhusu matukio mbalimbali na kuungua kwa masoko hayo.
“Minong’ono hiyo inaweza kuondolewa kupitia tu uchunguzi huru, kuhusu matukio hayo mbalimbali ya kuungua kwa masoko na kuharibu mali za wananchi,” amesema.
Kauli hiyo ya Semu imekuja siku chache baada ya Soko la wafanyabiashara wadogo Karume kuungua moto mara mbili ndani ya kipindi cha mwaka huu huku chanzo kikitajwa kuwa ni wafanyabiashara hao.
Awali tarehe 16 Januari, soko hilo liliteketea kwa moto huku chanzo kikidaiwa ni moto uliotokana na jiko la mkaa lililokuwa likitumiwa na wafanyabiashara hao licha ya kwamba uchunguzi wake bado haujathibitisha tukio hilo.
Tukio la pili lililotokea wiki iliyopita ilielezwa kuwa mfanyabiashara mmojawapo alikuwa anamuunganishia mwenzie umeme kwa njia ya kinyemela na kusababisha shoti ya umeme.
Vivyo hivyo katika masoko mengine ikiwa soko la wamachinga Mwenge na Soko Kuu la Kariakoo hadi sasa bado haijatolewa taarifa rasmi kuhusu kuungua kwa masoko hayo.
Leave a comment