WAKATI vyama vya siasa vya upinzani vikianza kutangaza ratiba ya kuanza mikutano ya hadhara, Chama cha ACT-Wazalendo kimesema Kamati yake Kuu, itakutana hivi karibuni kupanga mikakati ya utekelezaji wa suala hilo ili kije kwa kishindo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Jumamosi, tarehe 7 Januari 2023 na Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu, akizungumza na MwanaHALISI Online, kuhusu ruksa iliyotolewa hivi karibuni na Rais Samia Suluhu Hassan, kwa vyama vya siasa kufanya mikutano ya hadhara.
“Maamuzi ya kufunguliwa au kuondoa zuio la mikutano ya hadhara tumeyapokea na kwa chama chochote makini kwa uamuzi huo mnahitaji mkae chini kwenye vikao muweze kutoka na ratiba na utekelezaji ili mtoke kwa kishindo,” amesema Ado na kuongeza:
“Kamati Kuu itaitishwa katika siku chache zijazo na itatoa kalenda ya operesheni kuhusu mikutano ya hadhara.”
Kauli hiyo ya ACT-Wazalendo inakuja baada ya Chama cha Wananchi (CUF), kutangaza ratiba yake ya kufanya mikutano ya hadhara ambapo leo Jumamosi Mwenyekiti wake Prof. Ibrahim Lipumba, anatarajiwa kuzindua mkutano huo katika Viwanja vya Manzese Bakhresa, wilaya ya Ubungo, jijini Dar es Salaam.
Nacho Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimetangaza kuzindua mikutano ya hadhara kitaifa tarehe 21 Januari 2023, ingawa hakijataja eneo ambalo zoezi hilo litafanyika.
Leave a comment