CHAMA cha ACT-Wazalendo nchini Tanzania kimesema, kimeupokea kwa mikono miwili mwaliko uliitolewa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Kauli hiyo ya ACT-Wazalendo wameitoa leo Alhamisi tarehe 4 Juni 2020 ikiwa ni siku moja imepita tangu Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika atangaze kufungua milango ya ushirikiano kuelekea uchaguzi mkuu wa Oktoba 2020.
Jana Jumatano, Mnyika akizungumza na wanadishi wa habari makao makuu ya Chadema Kinondoni jijini Dar es Salaama alisema, wamefungua milango ya majadiliano na vyama vingine vya siasa ambavyo vinadhamira ya kweli ya kushirikiana kuiondoa CCM madarakani.
Leo Alhamisi tarehe 4 Juni 2020, MwanaHALISI ONLINE limezungumza na Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu juu ya kauli hiyo ya Chadema ambapo amesema, “ACT- Wazalendo tupo tayari kushirikiana na vyama makini vya upinzani.”
Tok Tok Tok…….. pic.twitter.com/yzZYy2yzDo
— Zitto MwamiRuyagwa Kabwe (@zittokabwe) June 3, 2020
“Tumeipokea kwa mikono miwili kauli ya Chadema kufungua milango ya ushirikiano,” amesema Shaibu
“Tunaamini hii ni dalili njema kuelekea kuwa na upinzani wenye nguvu kubwa ya kuikabili na kuing’oa CCM 2020,” ameongeza
Mwaka 2015, Chadema ilishirikiana na vyama vingine vitatu na kuunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ambao umoja huo ulianzia kwenye Bunge Maalum la Katiba mwaka 2014.
Vyama vingine vilikuwa ni NCCR-Mageuzi, CUF na NLD.
Nawasubiri kwa hamu sana. Siku 70 wataziona miaka 5. Wataongelea Vitu, tutazungumza na Watu kuhusu maisha Yao! Namwomba sana Mungu kwanza atupe uhai na pili atuondolee ubinafsi tuweze kuweka Nchi mbele, tunahitaji Umoja madhubuti wa Vyama 2 tu – @ACTwazalendo na @ChademaTz
— Zitto MwamiRuyagwa Kabwe (@zittokabwe) May 31, 2020
Kauli ya Shaibu inapewa nguvu na kile ambacho amewahi kukueleza Zitto Kabwe, Kiongozi wa ACT-Wazalendo kupitia akaunti yake ya Twitter akisema, katika uchaguzi ujao, unahitajika ushirikiano wa vyama viwili vya Chadema na ACT-Wazalendo.
Ugumu wa Ukawa wa mwaka 2015 kuendelea na mwaka huu unatokana na mazingira ya kinachoendelea ndani ya NCCR-Mageuzi na CUF.
Katika siku za hivi karibuni, NCCR-Mageuzi kimekuwa kikiwapokea viongozi na wanachama wa vyama vya upizania hususan kutoka Chadema huku wakirusha tuhuma kwa Chadema na viongozi wake, jambo ambalo linakuwa na ugumu kushirikiana.
Baadhi ya waliotangaza kutimkia NCCR-Mageuzi ni wabunge; Anthony Komu (Moshi Vijijini), Joseph Selasini (Rombo), Susan Maselle na Joyce Sokombi ambao ni wabunge wa viti maalum.
Kwa pamoja, wamesema, watahamia NCCR)-Mageuzi baada ya Bunge la Tanzania kuvunjwa.
CUF ambayo mwaka 2015 ilikuwa ikiongozwa na Mwenyekiti, Profesa Ibrahim Lipumba ambaye baadaye alijizulu katikati ya uchaguzi na lakini alirejea tena uchaguzi ulipomalizika, jambo ambalo wachambuzi wa kisiasa wamekuwa wakiliona hilo ni doa kwa CUF kushirikiana na Chadema.
Leave a comment