CHAMA cha Act-Wazalendo kimefunguka na kusema kwamba Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), haioni aibu kukandamiza demokrasia pamoja na uhuru wa vyombo vya habari, anaandika Faki Sosi.
Hayo yameelezwa leo na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Ado Shaibu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ambapo amesema kuwa kwa tathmini yao nchi ipo kwenye wakati mgumu Serikali ya CCM haioni aibu kukandamiza uhuru wa vyama vya siasa.
“Sasa kwa tathmini yetu Tanzania tunaishi katika zama ambazo Serikali ya CCM haioni aibu wala haina hofu kukandamiza misingi ya haki za kiraia na demokrasia ndizo zama tunazoishi,” amesema Shaibu.
“Ukifuata uelekeo kwenye mabadiliko ya sheria ya vyama vya siasa watu hawa watatuminya zaidi na tukiwaachia wanaweza kulala na kuamka na kuvifuta vyama vya siasa”
“Tunaishi zama ambazo Serikali ya CCM haina hofu wala soni kukandamiza uhuru wa mawazo, ukikosoa tu kwenye mitandao au kwenye vyombo vya habari unashughulikiwa “ amesema Shaibu.
Amesema kuwa kufungiwa kwa magazeti ni ishara ya kuminya uhuru wa habari.
Hivi karibu gazeti la wiki la MwanaHaLISI limefungiwa kwa muda wa miaka miwili pamoja na gazeti la Raia mwema kwa miezi mitatu.
Shaibu amesema kuwa uhuru wa mhimili wa Bunge umeminywa na mtu atakayejitokeza kutetea ananyamazishwa.
Leave a comment