CHAMA cha ACT-Wazalendo kinatarajia kufanya kikao cha Halmashauri Kuu tarehe 4 Septemba mwaka huu ambapo pamoja na mambo mengine kitaidhinisha jina la Mgombea wa Ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA). Anaripoti Felister Mwaipeta, TUDARCo … (endelea).
Pia kikao hicho kitakachohudhuriwa na viongozi mbalimbali, kitajadili mkakati wa chama hicho kuelekea Uchaguzi wa Serikali za mitaa utakaofanyika mwaka 2024 pamoja na uchaguzi mkuu mwaka 2025.
Hayo yameelezwa katika taarifa iliyotolewa leo tarehe 30 Agosti, 2022 na Naibu Katibu wa Habari, Uenezi na Mahusiano ya Umma ya chama hicho, Janeth Rithe.
Rithe alisema kikao hicho kikitanguliwa na vikao vya siku mbili vya Kamati kuu utakaofanyika tarehe mbili na tatu Septemba jijini Dar es Salaam.
“Kikao cha Halmashauri Kuu kitajadili ujenzi wa chama kuelekea Uchaguzi wa Serikali za mitaa 2024 na Uchaguzi mkuu wa 2025 hasa ikizingatiwa tumejipanga kikimilifu kuelekea uchaguzi huo,” alisema.
Leave a comment