CHAMA cha ACT-Wazalendo, kinatarajia kufanya maadhimisho ya kitaifa ya miaka nane ya kuzaliwa kwake, kesho Alhamisi, tarehe 5 Mei 2022, jijini Mwanza. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatano, tarehe 4 Mei 2022 na Naibu Katibu wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma ACT-Wazalendo, Janeth Rithe.
Taarifa ya Rithe imesema kuwa, maadhimisho hayo yatahudhuriwa na viongozi wakuu wa ACT-Wazalendo, ikiwemo Kiongozi wa chama hicho, Zitto Kabwe, Juma Duni Haji (Mwenyekiti), Dorothy Semu (Makamu Mwenyekiti Bara) na Ado Shaibu (Katibu Mkuu).
Katika maadhimisho hayo, chama hicho kitafanya shughuli mbalimbali za kijamii, ikiwemo uchangiaji damu salama, kuwajulia hali na kuwafariji wagonjwa na kupanda miti .
“Kama ilivyo ada, maadhimisho hayo yatafanyika kwa wananchama na viongozi wa chama kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii, ikiwemo kutoa damu, kuwajulia hali na kuwafariji wagonjwa, kupanda miti na kufanya usafi katika shule na hospitali,” imesema taarifa ya Rithe.
Taarifa ya Rithe imesema kuwa, tarehe 6 Mei 2022, viongozi wa ACT-Wazalendo na wanachama wa chama hicho Mwanza, watashiriki program ya uzinduzi wa ofisi za chama mkoani humo, majimbo na matawi.
Tarehe 7 Mei 2022, chama hicho kinatarajia kufanya kongamano la pili la Tume Huru ya Uchaguzi, kuelekea Katiba Mpya, jijini humo katika Ukumbi wa Hoteli ya Aspen.
Chama cha ACT-Wazalendo kilipata usajili tarehe 4 Mei 2022.
Leave a comment