ABDUL Nondo, Mwenyekiti wa Ngome ya Vijana wa ACT-Wazalendo, ametangaza nia ya kugombea ubunge Kigoma Mjini katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kigoma … (endelea).
Mbunge anayemaliza muda wake wa Jimbo hilo ni Zitto Kabwe ambaye haijafahamika kama atagombea tena ubunge au la ingawa Nondo amesema, yuko tayari kuvaa viatu vyake.
Zitto ambaye ni Kiongozi wa ACT-Wazalendo amekuwa mbunge wa jimbo hilo kuanzia mwaka 2015/20, kabla ya hapo alikuwa Kigoma Kaskazini.
Katika uchaguzi mkuu mwaka 2015, aliyekuwa mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba wa CCM alikwenda Kigoma Kaskazini alikokuwa Zitto na Zitto akahamia Kigoma Mjini na wote walishinda.
Leo Jumapili tarehe 5 Julai 2020, Nondo amesema ni siku muhimu kwake kueleza dhamira ya dhati kwa wakazi wa Jimbo la Kigoma mjini na wanachama wa ACT-Wazalendo ndani na nje ya Kigoma mjini.

“Kwamba, mimi Abdul Omary Nondo ninatangaza nia kwa dhati ya moyo wangu kugombea nafasi ya Ubunge Jimbo la Kigoma Mjini,” amesema Nondo.
“Sote tunafahamu uchaguzi ni mchakato, kutangaza nia ni hatua ya kwanza kidemokrasia, kuchukua na kurejesha fomu ni hatua ya pili kidemokrasia, kupitishwa au kutopitishwa na vikao vya chama (kura za maoni ) ni hatua ya tatu kidemokrasia.”
“Kuingia ulingoni kupeperusha bendera ya chama baada ya kuteuliwa na vikao vya chama ni hatua ya nne kidemokrasia, kuingia bungeni baada ya kupewa ridhaa na wananchi ni hatua ya tano na nyeti,” amesema Mwenyekiti huyo wa zamani wa Mtandao wa Wananchi Tanzania (TSNP).
“Hivyo, chama chetu kinaamini katika misingi 10 na msingi wa sana ni Msingi wa Demokrasia, kama kuwa huru kuchagua na kuchaguliwa. Kwa namna hiyo, vikao vya chama chetu ndio vitaamua nani wa kupeperusha bendera ya chama chetu Jimbo la Kigoma mjini,” amesema
Amesema, baada ya kazi na majukumu makubwa aliyoyafanya Zitto katika kipindi cha miaka mitano ya kuwatumikia wananchi wa Jimbo la Kigoma mjini, wakazi wa jimbo hilo bado wana fursa ya kuendelea kuchagua mbunge mwenye uwezo na ujasiri wa kuisimamia, kuikosoa na kuishauri serikali kikamilifu kwa maslahi ya wananchi.
“Wakazi wa Jimbo la Kigoma mjini bado wana fursa ya kuendelea kuchagua mbunge mwenye uwezo wa kuwasemea na kuwatetea muda wote panapotokea uonevu na dhulma dhidi ya wananchi.”
“Wakazi wa Jimbo la Kigoma mjini bado wana fursa ya kuendelea kuchagua mbunge mwepesi, mwenye uwezo na maono ya kutafuta na kubuni miradi mbalimbali kwa kushirikiana na manispaa kwa maslahi ya wananchi,” amesema
“Mimi Abdul Nondo, ikiwa nitafanikiwa kupitishwa na chama changu hakika nitakuwa mtu sahihi sana, mwenye utayari na uwezo wa kuvaa viatu vya Zitto Zuberi Kabwe kwa maslahi na maendeleo ya wananchi wa jimbo la Kigoma mjini,” amesema.
Leave a comment