RAMADHAN Kingai, aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Arusha, ameanza kutoa ushahidi katika Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhunumu Uchumi, kwenye shauri dogo la kesi ya msingi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka ya ugaidi, inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mbali na Mbowe, washtakiwa wengine kwenye kesi ya msingi ni, Halfan Bwire Hassan, Adam Kasekwa na Mohammed Abdilah Ling’wenya.
Kamanda Kingai ambaye sasa ni Kamanda wa Polisi, Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni (RPC), Dar es Salaam, ameanza kutoa ushahidi huo leo Jumatano, tarehe 15 Septemba 2021, mbele ya Jaji Mustapha Siyani.
Shauri hilo dogo linatokana na mapingamizi ya mawakili wa utetezi wakiongozwa na Peter Kibatala, kupinga Kamanda Kingai asitumie maelezo ya onyo ya mshtakiwa wa pili katika kesi hiyo, Adam Kasekwa kama kielelezo, kwa madai yalichukuliwa nje ya muda kisheria, pamoja na mshtakiwa kulazimishwa kuyatoa pasina hiari yake.
Mahojiano yao yalikuwa hivi;
Wakili Kidando: ACP Kingai, mshtakiwa wa pili Kasekwa analalamika kwamba aliteswa kabla na wakati akichukuliwa maelezo yake, unasemaje?
Kamanda Kingai: Siyo kweli, hakuteswa na wala hatukuwa na sababu za kumtesa.
Kama nilivyozungumza katika ushahidi wangu kwamba, hatukupata resistance kwenye ukamataji lakini pia baada ya kuwapata hao ilikuwa bado tunahitaji kupata kutoka kwao taarifa za wapi wenzao walipo.
Kwa hiyo, hatukuwa na sababu za kuwatesa sababu tungeweza pia kukosa tulichokuwa tunakifuatilia.
Wakili Kidando: Kwa sababu kuna malalamiko ya kuteswa, ili kuchukuliwa maelezo hayo uliyomhoji tueleze mazingira ya jinsi ulivyomkamata Moshi, mpaka kumfikisha Dar es Salaam na kumhoji?
Kamanda Kingai alianza kuulizwa maswali na mawakili upande wa Jamhuri, wakiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Robert Kidando, ambapo alidai mbele ya mahakama hiyo Kasekwa hakuteswa wakati anahojiwa kama ilivyodaiwa na mawakili wa utetezi.
Alipoulizwa na Wakili Kidando kuhusu malalamiko ya mtuhumiwa huyo kuteswa akihojiwa, Kamanda Kingai alidai Kasekwa hakuteswa wakati anahojiwa.
Kamanda Kingai alidai, mazingira ya mtuhumiwa kuchukuliwa maelezo yalikuwa rafiki.
Akiendelea kuulizwa na Wakili Kidando, Kamanda Kingai alidai, wakati anachukua maelezo ya Kasekwa alimhoji kwa kosa la kula njama za kufanya vitendo vya kigaidi, baada ya mtuhumiwa huyo kumueleza yupo tayari kuandika maelezo akiwa peke yake, pia aliyakubali kwa kusaini karatasi ya maelezo hayo.
Alipoulizwa kama mtuhumiwa alikuwa na hali nzuri kiafya wakati anamhoji, Kamanda Kingai alidai Kasekwa alikuwa na hali nzuri kiafya.
Wakili Kidando alipomuuliza kwa nini alichukua maelezo ya mtuhumiwa Dar es Salaam, badala ya Moshi mkoani Kilimanjaro alipokamatwa.
Kamanda Kingai alidai “kwanza kesi ilifunguliwa Dar es Salaam, ndipo ambapo taarifa pia imepokelewa na sehemu sahihi ambapo watuhumiwa wangeweza kuhojiwa, lakini tuliwatoa Moshi kuwaleta Dar es Salaam, kulikuwa na hatua nyingine za upelelezi ikiwa kuwakamata watuhumiwa wengine.”
Kamanda Kingai alidai, Kasekwa pamoja na mwenzake walichelewa kufikishwa Dar ea Salaam, kwa kuwa walikuwa wanawasaidia Polisi kumsaka mtuhumiwa mwingine aliyemtaja kwa jina la Moses Lujenge.
Pia, alidai Kasekwa wakati anapekuliwa baada ya kukamatwa, alikutwa na silaha aina ya pisto na dawa za kulevya.
Baada ya wakili Kidando kumaliza kumhoji Kamanda Kingai, Wakili Kibatala alianza kumhoji maswali.
Wakili Kibatala alimuuliza Kamanda Kingai kama alimuonya mtuhumiwa kuhusu kupatikana na silaha isivyo halali, ambaye alijibu akidai hakumuonya.
Baada ya shahidi huyo kutoa ushahidi huo, Jaji Siyani aliahirisha kesi hadi kesho Alhamisi, tarehe 16 Septemba 2021, ambapo upande wa Jamhuri utamalizia kumhoji.
Leave a comment