KIUNGO wa klabu ya Simba, Clatous Chama amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa wiki barani Afrika mara baada ya kuwashinda, Ricardo Goss wa Mamelodi Sundown, Amir Sayoud wa CR Belouizdad na Ferjani Sassi. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea).
Chama aliingia kwenye kinyang’anyiro hiko mara baada ya kuonyesha kiwango kizuri kwenye mchezo wa raundi ya tano ya hatua ya makundi ligi ya mabingwa barani Afrika dhidi ya As Vita kutoka Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo.
Katika mchezo huo klabu ya Simba, ilifanikiwa kuchomoka na ushindi wa mabao 4-1, hivyo kufuzu hatua ya robo fainali ya michuano hiyo kwa mara ya pili katika kipindi cha misimu mitatu ya Ligi.
Katika ushindi huo Chama alifanikiwa kupachika mabao mawili na kutoa pasi moja ya goli (Assist).
Kabla ya kinyang’anyiro hiko cha kupigiwa kura kufungwa, Chama alikuwa akiongoza kwa asilimia 51.
Licha ya kushinda tuzo hiyo, kiungo huyo amechaguliwa kuingia kwenye kikosi bora cha wiki cha Ligi ya Mabingwa barani Afrika.
Hii ni mara ya pili kwa Simba kutoa mchezaji bora wa wiki mara baada ya Luis Miquisone kuchaguliwa katika mzunguko wa pili wa hatua ya makundi ya Ligi ya mabingwa barani Afrika.
Leave a comment