MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Aboubakar Kunenge amesema, zaidi ya watu 49, wanashikiliwa na Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kwa tuhuma za wizi na ununuzi wa vifaa vya magari na pikipiki. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea).
Ni baada ya operesheni iliyofanywa na polisi chini ya kamanda wa polisi wa kanda hiyo, Lazaro Mambosasa, kukamata vifaa mbalimbali vya magari pamoja na pikipili zilizoibiwa.
Akitoa Mrejesho wa Operesheni, RC Kunenge amesema, kupitia msako uliofanyika wamefanikiwa kukamata vifaa mbalimbali ikiwemo taa za magari, Side mirror, power windows, Bampa, Vioo, Gearbox, Radio, Rim na vifaa vingine vingi.
Kutokana na hilo, Kunene amesema, kamwe hatoruhusu uhuni na wizi wa namna hiyo kuendelea mkoani mwake ambapo pia ametoa wito kwa wakuu wa mikoa wenzake kutokubali vifaa vya wizi kuuzwa katika mikoa yao.
Kwa upande wake, Kamanda Mambosasa amesema, miongoni mwa waliokamatwa ni wauzaji wa vifaa vya wizi ambao wamekuwa wakiwatuma wezi kwenda kuiba magari na vifaa.
Katika msako huo pia, wamefanikiwa kukamata gari iliyokuwa ikitumika kusafirisha vifaa vya wizi pamoja na Pikipiki zilizoibiwa.
Leave a comment