WATUMISHI wa taasisi mbalimbali za serikali wametakiwa kushiriki kikamilifu katika zoezi la usafi ambalo ufanyika kila jumamosi kuanzia saa moja kamili hadi saa tatu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hamasa hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Idara ya Mazingira na Mthibiti wa Taka ngumu katika Jiji la Dodoma, Dickson Kimaro muda mfupi baada ya kumalizika kwa zoezi la usafi.
Kimaro amesema kuwa watumishi wa serikali wamekuwa changamoto kubwa katika kushiriki shughuli za usafi licha ya kuwa ni jambo ambalo linafahamika.
Aidha amesema zoezi la usafi limekuwa likifanywa kila jumamosi ukiachilia jumamosi ya mwisho wa mwezi ambapo usafi ufanywa kwa kumuunga mkono Makamu wa Rais.
“Unaweza kuona hapa waliowengi ni akina mama na vijana lakini watumishi wa wengi wa serikali hawapo.
“Sisi watumishi wa umma tunatakiwa kuonesha mfano ndipo tutakuwa na ujasiri wa kuwahimiza wananchi kufanya usafi na kutii sheria pasipo shuruti,” amesema Kimaro.
Akizungumzia umuhimu wa kufanya usafi katika Jiji la Dodoma amesema kuwa ni kulifanya jiji kuwa la tofauti na lilivyokuwa Manispaa kwa lengo la kulifanya kuwa na mvuto wa aina yake.
“Licha ya Dodoma kuwa Jiji bado ni makao makuu hivyo ni wajibu wa kila Mwananchi mkazi wa Dodoma na ambaye siyo mkazi kuhakikisha anatunza mazingira na kulifanya jiji kuwa safi muda wote.
“Jambo lingine ni kupambana na magonjwa ya mlipuko ambayo yanaweza kujitokeza kama hapatakuwepo na usafi wa kutosha hasa magonjwa ya kuhara na mazalia ya mbu ambayo yanaweza kusababisha maralia au Dengue,” amesema Kimaro.
Mbali na hivyo amesema kuwa kwa sasa katika jiji la Dodoma hakuna changamoto ya ukosefu wa vyoo bora hata hivyo ameeleza kuwa bado kero ya ukosefu wa hupo maeneo ambayo bado hayajapimwa na wananchi kurasimishwa.
Pamoja na hayo Kimaro ameitaka jamii kuhakikisha inajenga vyoo bora na kushiriki kikamilifu katika utunzani wa mazingira kuanzia majumbani wanamoishi.
Leave a comment