NINAANDAMWA na dola. Ndiyo kauli ya Maalim Seif Shariff Hamad, Makamu wa Rais wa Kwanza katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ). Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Maalim Seif, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) na mwanachama namba moja wa Chama cha ACT-Wazalendo, ametoa kauli hiyo kwenye mahojiano maalumu na Kituo cha Televisheni cha Clouds, katika kipindi cha 360 leo tarehe Mosi Aprili 2019.
Maalim Seif alitoa kauli hiyo kutokana na kuulizwa kwamba, kwanini asianzishe chama chake baada ya kuondoka CUF na kuhamia Chama cha ACT-Wazalendo?
Kwenye mahojiano hayo Maalim Seif amesema, dola kwa maana ya Serikali ya Tanzania inamuandama na kwamba, hata kama angetaka kuanzisha chama baada ya kuondoka CUF, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa isingemkubalia.
Akifafanua Maalim Seif amedai kuwa, amekuwa akifanyiwa hujuma kubwa za kisiasa na kwamba, kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2015 visiwani Zanzibar alishinda, lakini ushindi wake uliporwa.
“Kwa msimamao wa msajili ninavyojua mimi, ningeanza kusema naunda chama change, nisingepewa usajili hata siku moja, asingenipa. Ninamsemea kwa sababu ya matendo ambayo amenifanyia tayari,” ameeleza Maalim Seif.
Hata hivyo, mwanasiasa huyo mkongwe na makini nchini amedai kuwa, pamoja na Jaji Francis Mutungi kumfanyia vitendo vyote hivyo, hana kinyongo naye.
“Nikimkuta msajili nitasalimia nae vizuri tu, sababu sina chuki na mtu. Nitamwambia msajili hebu tathimini ulichofanya ni haki, basi ‘simple’ tu,” amesema Maalim Seif.
Leave a comment