SERIKALI imeushauri Ushirika wa Kuweka na kukopa cha Polisi Tanzania (URA-SACCOS) kuona haja ya kuingia katika uwekezaji kwa kuanzisha viwanda vidogo vitakavyosaidia mambo mbalimbali. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Hayo yalibainishwa jana na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya ndani ya nchi, Kailima Ramadhani wakati akifungua mkutano mkuu wa 10 wa Saccos hiyo kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya mambo ya ndani ya nchi Meja Jenerali Jacob Kingu.
Kailima alisema, kuanzishwa kwa shughuli za uwekezaji kutasaidia Saccos hiyo kuendelea kufahamika zaidi, kuongeza ajira kwa vijana, kuongeza makusanyo ya kodi kwa Serikali na kufanya shughuli za maendeleo kuendelea kutekelezwa.
“Ni vyema ushirika huo ukatumia fedha katika kufanya miradi mbalimbali ikiwemo kufungua viwanda vidogo vidogo jambo ambalo litaongeza thamani ya chama, na kuunga mkono jitihada za Rais John Magufuli katika kukuza uchumi wa viwanda,” alisema Kailima.
Aidha alisema kuwa vyama vingi vya ushirika vimekua vikikumbwa na changamoto mbambali hivyo vinahitaji jitihada za ziada kupambana na changamoto hizo.
Alizitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na ushindani uliopo wa madeni ya taasisi nyingine za kifedha walionao watumishi wengi wanaoondolewa sifa ya kukopesheka kwa mujibu wa kanuni za utumishi wa umma, viwango vidogo vya uwekaji wa akiba kwa mwezi, upungufu wa mtaji, na baadhi ya wanachama kutokuwa na elimu ya kutosha ya masuala ya kiushirika na faida zake.
Awali Mwenyekiti wa bodi URA Saccos ambaye ni Kamishna wa Polisi, CP Albert Nyamhanga alisema Ushirika huo umefanikiwa kutoa mikopo kwa wananchama wake yenye thamani ya Sh. 185 bilioni tangu kuanzishwa kwake.
Mbali na mikopo hiyo tayari umeweza kukuza hisa zake hadi kufikia Sh. 6 bilioni huku kukiwa na ongezeko la akiba na amana zenye thamani ya sh. 39 bilioni hadi kufikia Septemba 30 mwaka huu.
Aidha alisema kuwa lengo la ushirika huo ni kuwa chachu kwa watumishi wa jeshi polisi ambao ni wanachama kuweza kutumia chombo hicho katika kujikwamua kiuchumi ikiwemo kupata fursa ya kuweka na kukopa fedha ili mwisho wa siku waweze kustaafu wakiwa na hali nzuri kimaisha.
Alisema kuwa lengo kuu la URA SACCOS ni kujenga mfuko imara wa kuwawezesha askari kujenga tabia ya kujiweka akiba, kuwawezesha wanachama kupata huduma za kibenki ambapo hadi hivi sasa ushirika huo umeweza kufungua matawi mengine katika maeneo ya Zanzibar, Mbeya, Tanga, Kigoma na maeneo mengine ili kuweza kuwafikia wananchama wake kwa ukaribu.
Kwa upande wake mnufaika wa ushirika huo, Safi Miraji kutoka tawi la Kaskazini Unguja alisema kuwa ameweza kunufaika na kujikwamua kiuchumi kwa kujenga nyumba na kusomesha watoto na hivyo kutoa wito kwa askari wengine kujiunga katika ushirika huo ili kuweza kujikwamua kiuchumi kupitia ushirika badala ya kukimbilia kwenye mabenki.
Leave a comment