BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) imepongeza hatua ya serikali ya kuboresha mfumo wa mauzo ya mazao ya wakulima hususani kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani ambao kwa kiasi kikubwa umeziwezesha taasisi mbalimbali za kifedha nchini ikiwemo benki hiyo kuweza kuwafikia wakulima kwa urahisi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hatua hiyo pamoja na mipango mingine, inatajwa kuwa imezirahisishia zaidi taasisi hizo kazi ya utoaji wa huduma mbalimbali za kifedha ikiwemo mikopo mbalimbali pamoja na elimu ya kifedha kwa wakulima.
Akizungumza kwenye kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Wakulima (Nane Nane) yaliyofanyika kitaifa jijini Dodoma leo, Mkuu wa kitengo cha wateja wadogo wadogo na wakulima kutoka Benki ya NBC, Raymond Urassa alisema kupitia maboresho makubwa kwenye mfumo wa mauzo ya mazao mbalimbali ya wakulima benki hiyo kama zilivyo taasisi nyingine za kifedha zimepata urahisi zaidi wa kuwatambua wakulima kama sekta inayoweza kukopesheka kupitia dhamana za malipo yao mbalimbali.
“Kupitia dhamana hii ya msingi kupitia mfumo thabiti wa mauzo ya mazao yao ndio sababu sasa sisi kama benki tumekuwa karibu zaidi na wakulima.’’ alisema Urassa.
“Kwasasa kupitia akaunti ya NBC Shambani wakulima wanaweza kupata mikopo ya nyumba bora, pembejeo na zana za kilimo bora zaidi ikiwemo matrekta, ‘power tiller’, mashine za kuvunia mazao yao yaani ‘combine harvester’, mikopo ya malipo ya awali wakati wanasubiri malipo na hivyo kuwatoa kuwatoa kwenye mikopo umiza ya mitaani. NBC tumeenda mbali zaidi kwasasa tunawasaidia wakulima kujenga maghala ya kutunzia mazao yao…tunaishukuru sana serikali kwa hili,’’ aliongeza
Zaidi Urassa aliongeza kuwa kupitia ukaribu wake na wakulima benki hiyo kwasasa imeweza kubuni huduma ya bima mbalimbali mahususi kwa wakulima na wafugaji ikiwemo bima ya afya, bima ya mifugo na bima ya kilimo huku ikiendelea kuingia mikataba na kampuni na taasisi mbalimbali nchini ili ziweze kuwakopesha wafugaji mbegu bora za mifugo ikiwemo ng’ombe, mbuzi, kondoo na kuku ili kuwasaidia wafugaji hao kuongeza uzalishaji wa nyama, maziwa na mayai.
Akizungumzia ukaribu uliopo sasa baina ya taasisi za kifedha hususani benki ya NBC na wadau wa sekta ya kilimo, Mwenyekiti wa Chama kikuu cha ushirika wilaya ya Tandahimba na Newala (TANECU) Karimu Chipola alisema umekuwa na msaada mkubwa kwao wakulima huku akitolea mfano namna wakulima wa korosho na ufuta kwenye mikoa ya Mtwara na Lindi walivyonufaika na mikopo ya zana za kilimo ikiwemo matrekta, mashine za kupulizia dawa ya wadudu, pikipiki, maguta na pamoja na elimu ya fedha kwa wakulima.
“Kiukweli tunaishukuru sana serikali kwa namna ambavyo inaendelea kutuweka karibu na taasisi hizi za kifedha ikiwemo NBC. Kwasasa imekuwa rahisi zaidi kwetu kama Union na AMCOS kuweza kufanikisha miamala ya malipo ya wanachama wetu kupitia akaunti zao. Zaidi kupitia ushirikiano wetu na NBC hivi karibuni tunakwenda kufanikisha mradi wetu wa ujenzi wa maghala makuwa ya kuhifadhia mazao pamoja na kujenga kiwanda chetu wenyewe cha kubangua korosho.’’ alisema.
Kauli ya Chipola iliungwa mkono na Bw Maiya Saitia Maumbi ambae ni mfugaji kutoka Wilaya ya Kilosa, mkoani Morogoro ambae kupitia maonesho hayo aliweza kukabidhiwa bima ya mifugo ya NBC kwa ajili ya mifugo yake.
“Kupitia bima hii nimeshashuhudia wafugaji wenzangu wakisaidiwa sana dhidi ya hasara zitokanazo na majanga kama ukame uliokithiri na magonjwa hatari ya mifugo. Kwasasa ninaweza kufuga kwa kujiamini nikiwa sina hofu yoyote kwasababu najua nimekingwa na bima ya uhakika kutoka NBC huku pia nikinufaika na huduma mahususi kwa wafugaji kupima akaunti ya wafugaji inayonihakikishia mikopo mbalimbali kwa ajili ya kuboresha shughuli zangu za ufugaji,’’ alisema Maiya.
Aidha, benki ya NBC imeyatumia vema maonesho hayo kwa kusogeza huduma zake mbalimbali kwa washiriki huku Meneja wa benki hiyo tawi la Dodoma, Happiness Kizigira akibainisha kuwa kupitia timu ya masoko ya benki hiyo kwa kushirikiana na mawakala mbalimbali wa benki hiyo jijini Dodoma.
ZINAZOFANANA
Mtihani mpya wagubika kesi za uwakilishi
TAMISA yataja maeneo 20 muhimu ya ‘kupiga pesa’ kwenye madini
Meridianbet wawashirikisha iMoon kuinogesha michezo ya kasino mtandaoni