WATU 14 ni wa familia moja kati ya 17, wamefariki dunia na wengine 12 wamejeruhiwa katika ajali ya gari iliyotokea eneo la Magira Gereza, Tarafa ya Mombo wilaya ya Korogwe mkoani Tanga. Anaripoti Mwandishi Wetu, Tanga… (endelea).
Miongoni mwa waliofariki, ni wanaume tisa na wanawake sita, wakiwamo watoto wawili mmoja wa kike na mmoja wa kiume.
Ajali hiyo ilitokea majira ya saa 4:30 usiku, eneo la Magila Gereza, katika barabara ya Segera – Buiko, lilihusisha gari aina ya Fuso na basi dogo aina ya Toyota Coaster, iliyokuwa ikitokea Dar es Salaam kuelekea Rombo, mkoani Kilimanjaro.
Basi hilo, lililokuwa na abiria 26, lilikuwa limebeba mwili wa Athanas Cosmass Mrema, aliyefariki dunia, katika maeneo ya Kimara, wilayani Ubungo, jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa mkoa wa Tanga, Omary Mgumba, alidai kuwa chanzo cha ajali hiyo, ni uzembe wa dereva wa lori wa kuendesha gari lake kasi kwa kutaka kulipita gari la mbele bila ya kuchukua tahadhari, hivyo kugongana uso kwa uso na basi hilo.
Kwa mujibu wa Mgumba, miili ya marehemu imehifadhiwa katika hospitali ya wilaya ya Korogwe; majeruhi 10 wamehamishiwa hospitali kuu ya mkoa wa Tanga (Bombo) na wawili wamebakishwa hospitali ya Korogwe kuendelea na matibabu.
Alisema, bado kuna miili ambayo haijatambulika.
Katika hatua nyingine, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulah, amefika asubuhi leo katika hospitali ya Bombo, kuwajulia hali majeruhi wa ajali hiyo. waliokuwemo kwenye basi dogo aina ya Toyota Coaster.
Leave a comment