WAKATI homa ya mtanange unaotarajiwa kupigwa kesho tarehe 22 Januari, 2022 kati ya Simba SC. na Mtibwa Sugar, mashabiki wa timu hizo wameshauriwa kupata chanjo ya UVIKO-19 kujishindia tiketi bure. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).
Wito huo umetolewa na Msemaji wa Mtibwa Sugar, Thobias Kifaru katika uwanja wa Manungu, Turiani mkoa Morogoro.
Kifaru amesema watu 10 wa kwanza kupata chanjo hizo watajishindia tiketi za kuushuhudia mchezo huo bure.
“Kwa kutambua umuhimu wa chanjo mimi nitakuwa mtu wa kwanza kupata chanjo, hivyo niwaombe na wananchi kupata chanjo kwa kuwa ina umuhimu mkubwa,” amesema Kifaru.
Aidha, Kifaru amesema baada ya kupata elimu juu ya UVIKO-19 ndipo alipofanya maamuzi ya kupata chanjo ili kujikinga mwenyewe na kukinga watu wake wa karibu.
Hata hivyo, Mtendaji Mkuu wa Timu ya Mtibwa Sugar, Swabri Aboubakar amesema hii ni fursa kwa mashabiki 10 wa kwanza kupata huduma ya chanjo kupatiwa tiketi za kuingia kutazama mchezo huo.
“Kwa kutambua juhudi za Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan na sisi kama viongozi tunawasihi wachezaji wetu na mashabiki wetu kupata chanjo ya UVIKO-19 ili tucheze kwa Furaha na kujiamini,” amesema Swabri.
Wakati mlinzi wa timu hiyo, Abdi Banda amesema alishapata chanjo baada ya kujua umuhimu wake ili ailinde familia yake.
“Mimi nimechanja kwa kujua umuhimu wake na wewe kachanje ili ujikinge mwenyewe na uwakinge wa karibu yako,” amesema Banda.
Leave a comment