MBUNGE wa Chadema katika jimbo la Singida Mashariki, Tundu Antiphas Lissu, amewasili salama nchini Ubegiji alikokwenda kwa ajili ya kupata matibabu zaidi. Anaripoti Saed Kubenea.… (endelea).
Taarifa kutoka kwa mmoja wa maofisa wa serikali nchini humo ambaye hakupenda kutajwa jina lake anasema, Lissu aliwasili kwenye uwanja wa ndege wa Zaventem, majira ya saa 11:40 ya jioni ya leo Jumamosi.
Mwanasiasa huyo machachari wa upinzani nchini, aliingia nchini humo kwa ndege ya shirika la ndege la Uholanzi (KLM), ambayo ilimchukua kutokea Amsadam, Uholanzi.
Lissu alianza safari yake ya matibabu ya tatu kutokea katika hospitali ya Nairobi, nchini Kenya.
Aliondoka Nairobi kwa ndege ya shirika la ndege la Kenya (KQ), majira ya saa mbili asubuhi ya leo Jumamosi.
Lissu alinusurika kifo tarehe 7 Septemba 2017, baada ya kushambuliwa kwa risasi na wanaoitwa na serikali, “watu wasiojulikana.” Tukio hilo lilitokea majira ya saa saba na nusu mchana, akiwa ndani ya gari, nje ya nyumba yake, katika eneo la Area D, mjini Dodoma.
Alikuwa akitokea bungeni alikokuwa anahudhuria mkutano wa Bunge. Waliomshambulia Lissu walitumia gari ina ya Nissan Patrol lenye rangi nyeupe.
Picha za gari ya Lissu aina ya Toyota Land Cruiser VX, zilizopigwa baada ya shambulio hilo, zinaonyesha gari la Lissu ambaye pia ni rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), likiwa na matundu zaidi ya 28 ya risasi.
Aidha, kwenye tairi la mbele la gari hilo, upande wa abiria, na sehemu nyingine kadhaa ambazo alikuwa amekaa mbunge huyo, kunaonekana kushambuliwa kwa risasi.
Kwa mujibu wa afisa huyo wa serikali ya Ubegiji, Lissu alipokelewa kwenye uwanja huo ndege wa kimataifa wa Zaventem, chini ya ulinzi mkali wa maofisa wa polisi na wale wa usalama.
Anasema, ulinzi umeimarishwa pia kwenye hospitali (jina tunalihifadhi), aliyopelekwa mwanasiasa huyo kwa ajili ya matibabu.
“Hapa kwenye uwanja wa ndege, tumeimarisha ulinzi kwa kuwa anayekuja nchini ni mmoja wa wanasiasa mashuhuri kwenye nchi anayotoka. Tumeimarisha pia ulinzi kwenye hospitali atakayotibiwa,” ameeleza afisa huyo.
Ameongeza, “tunapenda kuwahakikishia, tutafanya kila liwezekanalo kuhakikisha maisha ya Lissu muda wote atakapokuwa nchini kwetu, yanakuwa salama. Siyo yeye tu, hata mke wake na dereva wake.”

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Ubelgiji, serikali ya nchi hiyo imelazimika kuimarisha ulinzi baada ya kuombwa na watu waliokuwa wanaratibu safari na kufanikisha safari hiyo.
“Tulilazimika kuomba ulinzi baada ya kuwapo maneno mengi kutoka kwa baadhi ya watu waliokuwa wanakwamisha safari hii. Kuna wakati tulilazimika kuongea na maofisa wa ubalozi wa Ubelgiji mara kwa mara ili kupata hakikisho la usalama,” ameeleza mmoja wa watu waliofanikisha safari ya Lissu nchini Ubelghiji.
Anasema, “tulizungumza pia na serikali ya Jumuiya ya Ulaya. Wote walitupa ushirikiano wa kutosha na walituhakikisha maisha ya ndugu yetu kuwa yatakuwa salama. Hivyo unapoona ulinzi umeimarishwa kwenye viwanja vya ndege na hospitali, ni matunda ya maandalizi hayo.”
Kwa mujibu wa taarifa hizo, serikali ya Ubelgiji imeweka maofisa wa usalama wenye silaha kwenye hospitali ambayo Lissu anatibiwa.
Taarifa zinasema, hakuna mgeni yeyote anayeruhusiwa kuingia kwenye chumba ambacho amelazwa kwa ajili ya kumuona bila kuwa na kibali maalum cha hospitali na familia.
Lissu anatarajiwa kupatiwa matibabu zaidi nchini humo, ikiwamo kuangalia operesheni zilizofanyika Nairobi; risasi iliyosalia mwilini na kupata mazoezi ya kuanza kutembea tena.
Leave a comment