“Mimi napenda kuwa rais lakini ni suala la mazingira ya muktadha wa nchi wa sasa. Na kama wenzangu wataona kwa mazingira ya sasa Zitto anafaa kupambana na CCM, sitaukimbia msalaba huo,” amesema Zitto.
Amesema, hatua hiyo itafikiwa endapo muungano wa vyama wanaotarajia kuufuanya, utampa ridhaa hiyo.
Wakati akitoa kauli hiyo, Maalim Seif Sharif Hamada ambaye ni Mshauri Mkuu wa chama amesema, yupo tayari kugombea urais viziwani Zanzibar kwenye uchaguzi huo.
Wakizungumza katika mkutano na wanahabari leo tarehe 31 Desemba 2019, jijini Dar es Salaam kila mmoja amesema, watagombea nafasi hizo pale watakapoteuliwa kugombea.
Maalim Sief ameeleza kuwa, kwa sasa hana uhakika kama atagombea urais Zanzibar, lakini kama chama chake na Wazanzibari watampa ridhaa, atagombea.
“Mimi sijakata shauri kama nigombee au nisigombee, nategemea mazingira hayo,” amesema Maalim Seif ambaye amewahakikishia wafuasi wa chama hicho kwamba CCM itanag’olewa kwenye uchaguzi huo.
Akifafanua dhamira yake ya urais, Zitto amesema ndoto yake ni kuwa Rais wa Tanzania, na kwamba kama chama chake kitamteua kugombea nafasi hiyo kwenye uchaguzi mkuu wa 2020, atagombea.
“Ningependa kushiriki kwa dhati kuleta mabadiliko ambayo Watanzania wanapaswa kuwa nayo. Sasa hivi si suala la nani anakuwa mgombea.
“Ni jambo ambalo lazima wadau wote wanaotaka kuing’oa CCM madarakani. Inatakiwa kuangalia nani na kwa mazingira haya anafaa kubeba bendera ya kuiondoa,” amesema Zitto.
Amesema, anaumizwa na wimbi la umasiki linalowakabili Watanzania wengi, na kuahidi kwamba endapo atapata ridhaa ya kuwa Rais wa Tanzania, ataweka sera rafiki zitakazoleta maendeleo ya Watanzania.
“Mimi bianfsi naumizwa sana na hali ya maendeleo ya nchi yetu, naumizwa na ugumu wa maisha wananchi wanayopitia. Ugumu ambao haujasababisha na Mungu umesababishwa na sera fyongo za CCM. Ugumu huu wa maisha hatukustahili,” amesema Zitto.
Leave a comment