ZITTO Kabwe, Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo ameendesha maombi ‘maalum,’ kuliombea taifa kupitia ukurasa wake wa twitter. Anaripoti Hamis Mguta…(endelea).
Katika maombi hayo, Zitto amesema anaiona ndoto yake ya Tanzania kuwa yenye demokrasia madhubuti isiyo na ukiritimba.
“Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, nikiwa mnyenyekevu kwako nakuomba uendelee kunibariki na kuvuka mitihani ili kutimiza lile ulilonileta duniani kwalo.
“Uibariki nchi yetu Tanzania ivuke kipindi hiki kigumu katika historia yetu kama Taifa. Miezi michache hii iliyobaki utuvushe salama,” ameandika Zitto.
Andiko hiloa ameliweka leo tarehe 24 Septemba 2019, kwenye kumbukizi yake ya siku ya kuzaliwa ambapo anafikisha miaka 49.
“Sasa hivi katikati ya giza nene, naona ndoto hii ikitimia. Ni kama gari moshi kutoka Pwani kuelekea Bara likiwa limefika Kandaga (kabla ya kufika Kigoma Mjini) likiitafuta Kigoma.
“Kwa uwezo wa Mungu, nchi yetu itakomaa kidemokrasia. Mungu atazidi kutupa nguvu sote tulio kwenye upande wa haki, tutashinda,” ameandika Zitto.
Zitto amesema, ndoto za maisha yake imekuwa ni kuondoa ukiritimba wa chama kimoja nchini, na kwamba katika hilo hakuwahi kutetereka.
“Katika changamoto mbalimbali za siasa ambazo nimepitia, nikianguka, naamka, najipangusa, naendelea na safari ya kusaidia kuifanya nchi yetu kuwa na demokrasia madhubuti ya vyama vingi,” ameandika Zitto.
Leave a comment