ZIARA ya Rais John Magufuli mkoani Kigoma, imethibitisha kuwa Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT Wazalendo) ni kigeugeu, anayeweza kubadili kauli yake wakati wowote ili kukidhi mipango yake – haaminiki, anaandika Mwandishi Wetu.
Katika mkutano wa hadhara wa Rais Magufuli hadhara uliofanyika Kigoma mjini leo, Zitto ameipongeza Serikali ya awamu ya tano kwa kazi nzuri inayofanya huku akisema kuwa Rais Magufuli ameonesha njia kwa kuweka jiwe la msingi katika mradi wa maji.
“Mheshimiwa Rais hii ndiyo Kigoma, na watu wa Kigoma wanakukaribisha na wanakupenda sana kwasababu ya maendeleo. Tunakushukuru sana leo kwa uzinduzi wa mradi wa maji ambao utamaliza kabisa tatizo la maji katika mji wetu,” alisema Zitto.
Wakati Zitto akisema hayo leo, awali alitumia ukurasa wake Twitter kueleza kuwa ziara za Rais zinazofanyika ni usanii na kwamba hakuna mradi wowote mpya wa maendeleo uliopo mkoani Kigoma na kanda ya Magharibi kiujumla.
“Kuzifungua (barabara) ni usanii tu. Hakuna mradi mpya kanda ya Magharibi tangu Novemba 2015. Ni kuwahadaa wananchi tu na serikali inajua,” aliandika Zitto.
Hata hivyo, tofauti na ilivyotarajiwa katika mkutano wa leo Zitto ameishia kumpongeza Rais Magufuli na serikali ya awamu ya tano kwa uzinduzi wa mradi wa maji ambao umeanza 2013 na ulitakiwa kuisha mwaka 2015.
Zitto ameshiriki na kupongeza uzinduzi wa miradi ambayo hapo awali alisema ni ya “usanii tu” na yenye lengo la “kuhadaa wananchi.”
Leave a comment