HATUA ya Maalim Seif Shariff Hamad, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) kuhamia Chama cha ACT-Wazalendo, imepaisha chama hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mpaka sasa, ACT-Wazalendo kimevuna matawi 600 yaliyokuwa ya CUF visiwani Zanzibar muda mfupi baada ya Maalim Seif kuhamia chama hicho.
Pia jumla ya watu 125, 000 waliokuwa Wanachama wa CUF, wamepokea na kujiunga na ACT-Wazalendo na kaunza kufanya shughuli za chama hicho ikiwemo kupanga mikakati ya kujiimarisha.
Kauli hiyo imetolewa na Zitto Kabwe, Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo pia Mbunge wa Jimbo la Kigoma Mjini wakati akizungumza na wakazi wa Manispaa ya Kigoma Ujiji jana tarehe 1 Aprili 2019.
“Tayari visiwani Zanzibar jumla ya matawi 600 yaliyokuwa ya CUF yamekuwa ya Chama cha ACT-Wazalendo. Chama hiki ni kikubwa kwa sasa na ndio maana tunafanyiwa hujuma.
“Pamoja na mafanikio hao, tayari tuna wanachama zaidi ya 125,000 wapya waliokuwa wanachama wa CUF, wamejiunga na kuchukua kadi. Wapo wengi wanaoungana nasi lakini hawajaweza kupata kadi,” amesema Zitto.
Kiongozi huyo wa ACT-Wazalendo amesema, mafanikio hayo ni ya ndani ya wiki mbili baada ya Maalim Seif kujiunga na chama hicho na kwamba, wengine zaidi wataendelea kujiunga na kuchukua kadi za chama hicho.
Katika hatua nyingine Zitto amewaambia wakazi hao kuwa, iwapo tishio la Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini la kufuta chama hicho litatekelezwa, jimbo hilo litaathirika kwa kiwango kikubwa.
Amesema, Madiwani 19 na Kata 29 zitakosa wawakilishi ikiwa ni pamoja na Manispaa ya Kigoma Ujiji kuvunjwa kwa kuwa, waliopo hawawezi kukidhi asilimia 50 ya wawakilishi.
“Chama chetu kina madiwani 19 na kata 26 katika jimbo hili, iwapo tishio hili litatekelezwa, badi mimi mbunge pamoja na madiwani pia kata hizo kwa pamoja vitatoweka,” amesema Zitto na kuongeza;
“Ikiwa hivyo, jimbo hili na Mkoa wa Kigoma mtakosa mbunge wa kwenda kulilia matatizo yenu, mtakosa mtu wa kupaza sauti kwa ajili ya maisha yenu.”
Amesema, madiwani saba watakaobaki baada ya ACT-Wazalendo kufutwa, hawawezi kukidhi mahitaji ya kuendelea na vikao vya halmashauri kujadili miradi ya maendeleo ya jimbo hilo.
Leave a comment