KIONGOZI wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ameendelea kusota na safari za kwenda kuripoti katika kituo cha polisi cha Chang’ombe jijini Dar es Salaam, anaandika Hamis Mguta.
Kwa mara nyingine Zitto leo asubuhi ameripoti tena polisi siku ambayo wajumbe wa kamati kuu ya chama hicho nao wamefika katika polisi katika kitengo cha makosa ya fedha kwa ajili mahojiano kuhusu takwimu za uchumi.
Takwimu hizo zilitolewa na chama hicho hivi karibuni hatua ambayo imewaweka matatani.
“Nimeripoti na nimetakiwa kufika tena tarehe 17 mwezi huu, mahakama ndio itakayotoa tafsiri ya hili kwa sababu kuna wanasheria,” amesema Zitto.
Aidha, amesema kuwa chama kinaamini walichokifanya ni sahihi kwa kuwa walichokifanya ni kutafsiri na kuchambua takwimu zinazotolewa na ofisi ya taifa ya takwimu na hawakuongeza jambo.
Kadhia hii inahusisha baadhi ya maneno katika hotuba yake ya Oktoba 29, 2017 alipokuwa kwenye mkutano wa kuzindua kampeni za udiwani katika Kata ya Kijichi, wilayani Temeke jijini Dar es Salaam.
Moja ya matamshi yaliyomuweka Zitto matatani ni pamoja na kusema kwamba wananchi wasiichague CCM kwa sababu serikali yake imeshindwa kufanya uchunguzi na kuwakamata watu waliompiga risasi Mbunge Tundu Lissu mpaka siku hiyo.
Kadhalika Zitto anadaiwa kuwataka wananchi wasiichague CCM kwa sababu serikali yake imeshindwa kueleza chanzo cha miili ya watu wanaookotwa kwenye fukwe za bahari kama Coco Beach.
Hivyo Zitto akasema kuichagua CCM ni sawa na kuwaunga mkono waliofanya vitendo vya kumshambulia Tundu Lissu na wanaoua watu wanaookotwa kwenye fukwe.
Zitto aliongozana na timu ya wakili wa chama pamoja na mke wake katika kituo hicho cha Chang’ombe jijini Dar es Salaam.
Baada ya kutoka kituoni hapo alielekea kituo Kituo cha Polisi Kamata, ambapo kaimu Mwenyekiti wa Chama, Yeremiah Maganja, pamoja na Katibu Mkuu, ndugu Dorothy Semu, wameitikia wito wa Kamishna wa Makosa ya Jinai (DCI) wa Jeshi la Polisi kituoni hapo ambapo hadi sasa bado wanaendelea na mahojiano.
Leave a comment