ZITTO Kabwe, Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo ametoa wito kwa viongozi wa dini kukemea vitendo vya baadhi ya viongozi wa siasa, wanaohatarisha amani ya nchi. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Zitto ametoa wito huo leo tarehe 27 Julai 2019 katika harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa la EAGT lililoko Yombo Kilakala wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika harambee hiyo, Zitto amesema viongozi wa dini wana wajibu wa kuonya, kukemea na kuwaasa waumini wao wakiwemo viongozi ili kulinda na kudumisha amani.
“Nyie viongozi wa dini mna wajibu mkuu zaidi kwa taifa, maana siye ni waumini wenu katika nyumba zenu za Ibada mnayo nafasi ya kuonya, kukemea na kuleta suluhu na muafaka wa kitaifa. Mnayo nafasi ya kutuweka pamoja viongozi na tukajadili njia bora za kulinda na kudumisha amani ya nchi yetu, nawahimiza msiache wajibu wenu huu,” amesema Zitto.
Zitto amesema msingi wa amani ya taifa kwa sasa unashambuliwa. “Msingi mkuu wa amani yetu ni utamaduni wetu wa kisiasa na kiuchumi ambao sasa unashambuliwa, na ni dhahiri watawala ndiyo vinara wa mashambulizi hayo. Utamaduni wetu wa kiuchumi sasa upo kwenye tishio kubwa na hivyo amani yetu ipo kwenye tishio kubwa sana,” amesema Zitto..
Zitto ameeleza kuwa, kwa sasa nchi inakabiliwa na vitendo vya dhuluma, chuki, vijana wengi wasio na ajira na matumizi mabaya ya madaraka, hali ambayo inahatarisha amani.
“Taarifa za tafiti mbalimbali juu ya asili ya amani ya nchi yetu zinaonyesha kuwa sababu zote zinazopelekea nchi nyengine jirani kutokuwa na amani zipo pia hapa Tanzania. Ukosefu wa haki, udini, ukabila, dhuruma, udikteta, umasikini, chuki, hali mbaya ya uchumi, matumizi mabaya ya madaraka na uwepo wa vijana wengi wasio na ajira,” amesema Zitto na kuongeza.
“Sababu zote hizi zipo Tanzania, lakini nchi yetu haina uvunjifu mkubwa wa amani. Kwanini? Tanzania ina amani kwa sababu ya Sera na Mienendo ya Viongozi waasisi wa Taifa letu vilisaidia kuunda utamaduni wa kiuchumi na kisiasa uliojikita kwenye utu, usawa, upendo na umoja, vilivyozaa amani amani ya nchi yetu.”
Zitto amewataka viongozi wa dini kuwahimiza Watanzania kuepuka vitendo vitakavyo leta ubaguzi na matabaka kwa misingi ya vyama vya siasa, ukabila na dini, ili kuimarisha uhuru wa kila mtu. Pamoja na kukomesha vitisho kwa watu wanaotumia haki zao kikatiba kutoa mawazo mbadala.
“Siku tutakayoshindwa kabisa kufanya hayo, uhasama utazidi, mpasuko utapanuka, wananchi wetu watapoteza matumaini ya kuwa nchi hii ni moja na kila raia anayo haki bila kujali tofauti zote za kisiasa, kiuchumi, kidini na kikabila, na mwishowe nchi hii itapasuka vipande vipande, na amani yetu kutoweka,” amesema Zitto.
Leave a comment