ZITTO Kabwe, Kiongozi wa Chama cha ACT- Wazalendo, ameunda timu ya watu kumi ili kuandaa Ilani ya Uchaguzi Mkuu 2020/2025. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea)
Taarifa ya Zitto aliyoitoa leo Jumamosi tarehe 23 Mei, 2020 imesema, timu hiyo itaongozwa na mwanataalamu, Mwanahamisi Singano na Katibu atakuwa, Idrisa Kweweta ambaye ni katibu wa sera, utafiti na mafunzo wa chama hicho.
Zitto amesema, timu hiyo itachambua maoni ya wananchi yaliyokusanywa nchi nzima wakati wa “listening Tour” na kuandaa Rasmi ya Ilani ya mwaka 2020.
“Rasimu hii ya ilani itakayoandaliwa (pamoja na ile ya Zanzibar), zitafikishwa kwenye sekretarieti, kamati kuu na halmashauri kuu ya taifa ya chama ili kuidhinishwa,” amesema Zitto
Zitto ambaye pia ni mbunge wa Kigoma Mjini amesema, “naitakia timu hii kila la kheri katika utekelezaji wa majukumu yao haya.”
Wajumbe wengine katika timu hiyo ni; Emmanuel Mvula, wakili na mtaala wa haki za kijamii; Dk. Elizabeth Benedict, mtaalamu sekta ya afya; Godluck Mushi, mtaalamu sekta ya fedha na Ismail Jussa ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu.
Wengine ni, Abdul Nondo, Mwenyekiti wa Ngome ya Vijana wa ACT-Wazalendo; Dk.Janeth Fussi, Katibu wa Ngome ya Wanawake wa chama hicho; Mwanaisha Mndeme, Katibu wa Ngome ya Vijana wa chama hicho na Edgar Mkosamali ambaye ni katibu wa idara ya bunge na baraza la wawakilishi wa ACT-Wazalendo.
Leave a comment