ZITTO Kabwe, Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, amemtaka Prof. Palamagamba Kabudi, kujiuzulu uwaziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kwa madai ya kufeli kuendesha sera za mambo ya nje. Anaripoti Martini Kamote … (endelea).
Zitto ametoa ushauri huo leo tarehe 5 Desemba 2019, wakati akihojiwa na Kituo cha ITV kupitia Chaneli yake ya YouTube.
Kiongozi huyo wa ACT-Wazalendo ametaka Prof. Kabudi kujiuzulu, kufuatia hatua ya ndege za Serikali ya Tanzania, kushikiliwa nje ya nchi kutokana na kesi za madai, na kwamba suala hilo linatokana na nchi kuwa na sera mbovu za mambo ya nje.
“Suala la ndege tulisema hatutalizungumza, lakini sasa hii imezidi, Wizara ya Mambo ya Nje imeonesha namna gani imefeli kutekeleza sera ya mambo ya nje. Na hakika ningemuomba Mwalimu wangu Prof. Kabudi ajiuzulu,” ameshauri Zitto.
Ameeleza kuwa, Prof. Kabudi anatakiwa ajiuzulu ili atafutwe waziri mwingine atakayeweza kuondoa changamoto zilizopo, ili nchi isikutane tena na dhahama kama hiyo
Zitto ameeleza, katika uongozi wa Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Rais Jakaya Kikwete, walikuwa na maarifa katika kushughulikia kesi za madai ili kuepusha mali za nchi kushikiliwa nje ya nchi na wadaiwa wake.
“Sio kwamba utawala wa Kikwete haukuwa na kesi, lakini walikuwa na maarifa ya kushughulikia kesi zisifikie mahali ambapo mali za nchi zinaweza zikakamtwa. Inaonesha tosha ni namna gani tunaendesha sera zetu za mambo ya nje,” amesema Zitto.
Hivi karibuni ndege ya Serikali ya Tanzania ilishikiliwa nchini Canada kwa amri ya mahakama iliyotokana na kesi ya madai iliyofunguliwa na Hermanus Steyn. Ni mara ya pili kwa ndege ya Tanzania kushikiliwa nchini humo kutokana na kesi za madai.
Leave a comment