ZITTO Kabwe, Kiongozi wa Chama cha siasa cha ACT-Wazalendo nchini Tanzania, ameweka wazi msimamo wa chama hicho kuwa hakitasusia Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Faki Sosi, Rufiji … (endelea).
Akizungumza na wananchi katika jimbo la Rufiji mkoani Pwani jana Jumatatu tarehe 22 Juni 2020, Zitto alisema, chama hakitarejea nyuma kwenye uchaguzi huo hata kama kinakwenda kwenye uchaguzi huo kwenye mazingira magumu.
“Wanaweza kufanya kama walivyofanya katika uchaguzi wa serikali za mitaaa (uliofanyika tarehe 24 Novemba 2019) wakazuia kampeni, mnafahamu bunge lenu lilizimwa ili kuzuia mawazo mbadala ya upinzani,” alisema.
Zitto alisema, tayari chama hicho kimechukua tahadhari Na kimekutana na jumuiya za kimataifa kuieleza hali iliyotokea kwenye chaguzi za marudio na ule wa serikali za mitaa wa mwaka 2019.
“Wanaweza kujaribu kufanya hivyo tena lakini sisi tunaweza kuzuia hilo, tumeshaeleza jumuiya ya kimataifa ili kuthibiti hali hiyo, ni lazima na sisi kuchukua hatua ili dunia ione kwamba kweli wananchi wamekataa,” alisema Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Mjini
“Licha ya mataifa kadhaa kuweka vikwazo na kutoutambua uchaguzi wa Zanzibar lakini hakuna kilichobadilika Serikali imeshupaza shingo.”
“Tujipange kufanya mabadiliko ya kisiasa katika nchi, najua tuna hofu lakini tuondoe hofu tupambane hakuna njia ya kumwambia mtawala kuwa tumekasirika lakini kwa karatasi ya kura
“Tutadaia tume huru ya uchaguzi huku tunashiriki uchaguzi na tutashiriki uchaguzi huku tunadai tume huru,” alisema.
Aliwataka wagombea wa nafasi zote kwenye uchaguzi Mkuu kujaza fomu za kugombea kwa umakini.
“Tutawaandaa wagombea wetu kuhakikisha hatutoi mwanya wa wagombea wetu kuenguliwa, tunafahamu tume si huru lakini tutashiriki na tutashinda, CCM wanafanya hujuma kuhakikisha tunasusia uchaguzi nashauri tusisusie,” alisema.
“Kule kwangu Kigoma wameweka timu kubwa kuhakikisha Zitto harudi bungeni lakini hawasemi kuwa watashinda lakini watu wa Kigoma wameshawaonya kuwa kama Zitto atagombea ubunge Kigoma mthubutu kutomtangaza kwa hio kuweni na ujasiri kama huo,” amesema
Katika Ziara hiyo, Zitto amepokeo madiwani wanne kwenye Halmashauri ya Rifiji waliokuwa madiwani kupitia Chama cha Wananchi CUF ambao ni pamoja na, Juma Mlanzi Diwani kata ya Umwe, Issa Miduma kata ya kipugila, Hassan Mpota kata ya Mgomba, Sofia Mkengesi viti maalum.
Leave a comment