VIKAO vya Kamati ya Bunge vinaanza wiki ijayo ambapo miongoni mwa kazi zitazofanywa ni pamoja na kupitia na kuchambua Taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG). Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Ndani ya taarifa ya CAG kuna upotevu wa Sh. 1.5 trilioni ambazo zimezua mjadala mkubwa nchi ambapo mpaka sasa, haijaelezwa zimetumikaje.
Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na ile Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) zitachambua taarifa hiyo ya CAG kwa mwaka 2016/17 unaoishia Juni 30.
Taarifa ya kuanza kwa vikao vya bunge imetolewa na Kitengo cha Habari, Elimu kwa Umma na Mawasiliano cha Ofisi ya Bunge na kwamba, vikao hivyo vinatarajiwa kuanza Agosti 20 hadi 31, mwaka huu.
Vikao hivyo vinatakiwa kuanza kufanyika kabla ya Vikao vya Mkutano wa 12 wa Bunge kuanza tarehe 4 Septemba mwaka huu.
Kutokana na uchambuzi huo wa kamati hizo zinazosimamia matumizi ya fedha za umma, hauwezi kukwepa kugusa suala lililoibua mjadala mkali kupitia ripoti ya CAG ikidaiwa kuwa Sh trilioni 1.5 hazijulikani ziliko.
Mwanasiasa Zitto Kabwe, ambaye ni Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), ndiye aliyeibua suala hilo na kulivalia njuga wakati wa vikao vya Bunge la Bajeti.
Zitto, aliyedai kutumia ripoti ile ile ya CAG inayoishia Juni 30, mwaka jana, alihoji ziliko Sh trilioni 1.5.
Hata hivyo, hoja ya Zitto ilijibiwa Aprili 20, mwaka huu na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji, aliyefafanua kuwa, katika fedha hizo kiasi cha Sh bilioni 697 kilitumika kwa matumizi ya dhamana na hati fungani zilizoiva na Sh bilioni 687 kilikuwa kwa ajili ya mapato tarajiwa.
Pia alisema kiasi cha Sh bilioni 203 kilikusanywa kama kodi kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ).
Baada ya sakata hilo kuibuliwa tena bungeni Juni 5, mwaka huu na wabunge wa Chadema, Halima Mdee (Kawe) na John Mnyika (Kibamba) kulisababisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu), Jenista Mhagama, kuwataka wabunge kutojadili kuhusu fedha hizo ndani ya Bunge hadi hapo PAC inayoifanyia kazi itakapowasilisha ripoti yake.
Kutokana na sakata hilo, Rais Dk. John Magufuli alimhoji CAG, Profesa Musa Assad na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Dotto James, kuhusu ukweli wa madai ya upotevu wa fedha wakati alipowaapisha majaji wapya walioteuliwa Ikulu, Dar es Salaam na wote kwa pamoja walikanusha.
Leave a comment