MATUKIO yaliyotikisa katika Uchaguzi Mdogo wa udiwani na ubunge sasa yameanza kuhojiwa bungeni. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea)
Miongoni mwa matukio hayo ni madai ya baadhi ya wagombea wa upinzani kunyimwa fomu, wakurugenzi wa uchaguzi kudaiwa kukimbia ofisi wakikwepa kupokea fomu za wagombea, pamoja na matukio ya majaribio ya utekwaji kwa baadhi ya wagombea hasa wa upinzani.
Akiuliza swali katika mkutano wa kumi na mbili wa Bunge, kikao cha kwanza leo tarehe 4 Septemba, 2018 bungeni jijini Dodoma, Mbunge wa Serengeti Marwa Lyoba Chacha (Chadema), amehoji kuhusu matukio hayo akidai kuwa yanaashiria kwamba hakuna tume huru ya uchaguzi.
Akijibu swali la Chacha, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Anthony Mavunde amesema kuwa, matukio hayo hayaashirii kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) haiko huru, kwa kuwa haijakiuka majukumu yake kwa mujibu wa katiba ya nchi ibara ya 74 ibara ndogo ya kwanza.
Akifafanua kuhusu madai hayo, Waziri Mavunde ameeleza kuwa, NEC tangu kuanzishwa kwake majukumu yake ni kuratibu na kusimamia shughuli za uchaguzi, na kwamba hadi sasa imesimamia chaguzi tano za urais na chaguzi ndogo mbalimbali kwa ufanisi na hivyo iko huru.
“Tume ya uchaguzi imeanzishwa kwa mujibu wa ibara ya 74 ya ibara ndogo ya kwanza, katiba ambayo imeonyesha majukumu ya tume ya uchaguzi katika kutekeleza wajibu wake. Tangu kuanzishwa vyama vingi mwaka 1992 imeendesha chaguzi tano za urais na chaguzi ndogo mbalimbali na imefanya kwa ufanisi kwa hivyo tume iko huru,” amesema na kuongeza.
“Unaipimaje tume ni huru, unaipima kutokana na majukumu yake yaliyoko kwa mujibu wa katiba, katiba imeanisha majukumu ya tume ya uchaguzi ambapo kwa msingi, jukumu ni kuendesha utaratibu wa uchaguzi, kama watu wametekwa hilo ni kosa la kijinai ungeenda kuripoti polisi.”
Leave a comment