HAMID Hemed Salum (39) na Saidi Hemed Salum (40) wamekamatwa na Wakala wa Dawa, Chakula na Vipodozi Zanzibar (ZDFA), kwa tuhuma za kuuzia wateja juisi ya tende iliyochanganywa na dawa za kuongeza nguvu za kiume kisiwani Unguja. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Akizungumzia kuhusu sakata hilo, Nassir Ali Buheti, Kaimu Mkurugenzi wa Wakala wa Dawa, Chakula na Vipodozi Zanzibar (ZDFA) amesema, wamekamatwa na maofisa wa wakala huo, baada ya kubainika kuuza juisi hiyo kwa zaidi ya miezi sita.
Buheti ameeleza kuwa, baada ya ZDFA kupata tetesi za watuhumiwa hao kuuza juisi ya tende yenye dawa za kuongeza nguvu za kiume, wakala huo ulituma ofisa wake kwa ajili ya kufanya uchunguzi.
“Nilipata taarifa kwamba kuna mfanyabaishara anafanyabiashara katika gari, anauza juisi ya tende lakini pia anauza dawa ya kuongeza nguvu za kiume,” amesema Buheti.
Amesema, baada ya ofisa wake kufika eneo la wafanyabishara hao, aliuziwa juisi ya tende iliyochanganywa na dawa ya kuongeza nguvu za kiume.
“Tulituma ofisa wetu kwa ajili ya kuchunguza, akauziwa juisi ya tende iliyo na dawa ya kuongeza nguvu za kiume na kupewa namba kama akihitaji tena,” amesema Buheti.
Amesema, kitendo kilichofanywa na wafanyabiashara hayo ili kuvutia wateja, ni hatari kwa afya ya binaadamu.
Mtuhumiwa Salum amesema, dawa hizo huchukua kutoka kwenye maduka la dawa akitaja kuwa ni Viagra na kuzichanganya katika juisi hiyo.
Leave a comment