SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), imetangaza ongezeko la wagonjwa wapya sita wa Homa Kali ya Mapafu inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19). Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Taarifa ya ongezeko hilo imetolewa leo tarehe 15 Aprili 2020, na Hamad Rashid Mohammed, Waziri wa Afya Zanzibar.
Taarifa ya Mohammed inaeleza kuwa, kufuatia ongezeko hilo, kwa sasa Zanzibar ina jumla ya wagonjwa 18 kutoka idadi ya watu 12 iliyokuwepo awali.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, wagonjwa watano ni raia wa Tanzania ambao hawana historia ya kusafiri nje ya nchi siku za hivi karibuni, na mmoja ni raia wa Misri, aliyeingia nchini akitokea kwao kupitia Dubai kwa Shirika la Ndege la Fly Dubai.
Mohammed amesema wagonjwa wote wamelazwa katika vituo maalumu kwa ajili ya kuendelea na matibabu.
“Serikali kupitia wizara ya afya inaendelea kuwasisitiza wananchi kuchukua tahadhari zote za kujikinga na ugonjwa huu zinazotolewa mara kwa mara ikiwemo unawaji mikono kwa maji yanayotiririka na sabuyni , kuepuka misongamano na kuahirisha safari za nje na ndani ya nchi zisizo za lazima,” inaeleza taarifa ya Mohammed.
Leave a comment