SHIRIKISHO la mpira wa miguu Tanzania (TFF), kupitia katibu mkuu wake Wilfred Kidao imesema mpaka sasa hawajajua watatoa zawadi ipi kwa bingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara kwa msimu huu kutokana na ligi hiyo kutokuwa na mdhamini kwa sasa. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Hali hiyo imekuja baada ya aliyekuwa mdhamini wa ligi hiyo kampuni ya simu ya mkononi ya Vodacom kujiondoa katika udhamini wa ligi hiyo kwa msimu huu licha ya mazunguzo baina ya TFF na kampuni hiyo kuendelea kabla ya kutoka kwa taarifa kamili.
Katibu mkuu huyo amesema shirikisho hilo bado lipo katika mchakato wa kusaka mdhamini mwingine baada ya kuwa katika mazungumzo na makampuni mbalimbali ya kibiashara.
“Viongozi wa taasisi na mimi hatulali tunafanya kazi kubwa kubwa kuhakikisha mzunguko wa ligi wa raundi ya 6, 7 au 8 tunapata mdhamini mkuu lakini kupata co-sponsors ni kitu kikubwa zaidi kwa sababu tutapata watu wadogo wadogo lakini wengi ligi itakuwa na thamani kubwa,” amesema Kidao.
Kujiondoa kwa wadhamini katika ligi hiyo kumeendelea kufanya klabu nyingi zinazoshiriki Ligi Kuu kuwa katika hali mbaya ya uchumi kwa kuwa na vyanzo vichache vya mapato kama matangazo ya televisheni kupitia Azam TV na mapato ya mlangoni ‘Gate collection’.
Ikumbukwe hapo awali mdhamini mkuu alikuwa anatoa zawadi ya kombe pamoja na pesa taslimu Sh. 81.3 milioni, kwa bingwa wa Ligi Kuu, mshindi wa pili alijinyakulia Sh. 40 milioni, mshindi wa tatu alikuwa anaondoka na Sh. 29 milioni na wa nne Sh. 23,241,635.
Kwa upande wa mchezaji bora, mfungaji bora na kipa bora kila mmoja alikuwa anaondoka na kitita cha Sh 5,742,940 huku mwamuzi bora na kocha bora kila mmoja alichukua Sh 8,614,610 wakati timu yenye nidhami ilikuwa inapata Sh. 17 milioni.
Leave a comment