MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, Beatrice Dominic, amekiri kumuandikia barua Naibu Meya, Ramadhan Kwangaya, kukabidhiwa majukumu yote ya Umeya ndani ya Manispaa hiyo. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Kwangaya anachukua nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Ubungo, Boniface Jacob.
Taarifa kutoka ndani ya Manispaa hiyo zinasema, hatua ya mkurugenzi ya kumtaka Kwangaya kushika mikoba ya kuendesha na kusimamia shughuli za manispaa hiyo, imetokana na kujiridhisha kuwa Jacob amepoteza sifa ya kuwa diwani wa Kata ya Ubungo.
Jacob alitangazwa kuvuliwa uanachama wa Chadema na Kamati Tendaji ya Kata ya Ubungo, tarehe 28 Aprili mwaka huu, kwa kile walichokieleza kuwa utovu wa nidhamu na kutengeneza makundi chonganishi ndani ya chama.
Tuhuma nyingine zinazodaiwa kusababisha Jacob kufukuzwa uwanachama, ni kuwatumia baadhi ya vijana wake, akiwamo Betha Mwakasege, kuwatukana na kushambulia baadhi ya viongozi wa chama kwa matusi.
Kwangaya ni Diwani wa Kata ya Manzese kupitia Chama cha Wananchi (CUF); chama cake kina madiwani watatu kwenye manispaa hiyo. Ameweza kuwa naibu meya wa manispaa hiyo, kufuatia ushirikiano uliokuwapo wa vyama vya upinzani kwenye uchaguzi mkuu uliyopita, maarufu kama UKAWA.
Akizungumza na MwanaHALISI ONLINE, leo Jumatano, tarehe 6 Mei 2020, Betrice amesema, amempa barua Kwangaya ya kukaimu nafasi hiyo ili kuruhusu shughuli za manispaa kuendelea kama kawaida.
Naye Kwangaya amekiri kupata taarifa ya kuwapo barua ya kukaimishwa nafasi hiyo.
Alisema, “ndio muda huu, nimepokea simu kutoka kwa mkurugenzi, inayonitaarifu kuwa kuna barua yangu inayonikaimisha Umeya wa Ubungo. Naomba niipokee, kisha nitazungumza na wewe.”
Wakati huo, Kwanganya alisema, alikuwa akihudhuria mazishi ya Sheikh Suleiman Kilemile, ambaye amefariki duania usiku wa kuamakia leo Jumatano jijini Dar es Salaam.
Akiandika katika ukurasa wake wa twitter, Jacob ameeleza “kiani” hatima ya umeya wake kwa kusema, uamuzi huo hauna athari kwa upinzani kwa kuwa aliyekaimishwa ni mpinzani hivyo bado Manispaa hiyo ipo mikononi mwa upinzani.
“Naomba niwahakikishie kuwa, Manispaa ya Ubungo bado ipo katika mikono yetu salama ya Chadema + CUF, Naibu Meya (mpinzani), kamati ya fedha CCM 1 kati ya wajumbe 9 na Baraza la wajumbe 22, CCM wapo 6 tu. Hata kama wataniondoa mimi CCM hawanufaiki kwa lolote. Swali-Why Me na why Now,” ameeleza.
Leave a comment